Mnara
wa Kumbukumbu ya Mashujaa baada ya kuwekwa kwa silaha za asili za mashujaa na
maua
|
Baadhi
ya wananchi wakifuatilia shughuli ya maadhimisho ya Siku ya kumbukumbu ya
Mashujaa Tanzania katika viwanja vya Mashujaa vilivyopo mjini Dodoma.
(Picha na Hassan Silayo)
|
Na: Immaculate Makilika- Dodoma
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amewaasa watanzania kudumisha amani iliyopo
ambayo ilipatikana baada ya Mashujaa mbalimbali kuipigania na hata kujitoa uhai
wao kwa ajili ya Taifa.
Akizungumza leo, wakati akihutubia wananchi mara
baada ya kumaliza shughuli za maadhimisho ya Siku ya kumbukumbu ya
Mashujaa iliyofanyika katika viwanja vya
Mashujaa vilivyopo mjini Dodoma.
Rais Magufuli alisema kuwa maadhimisho ya
kumbukumbu za Mashujaa ni muhimu kwa
vile watu hao walijotoa kwa ajili ya kulitetea taifa.
“Wakati tunawakumbuka waliotangulia mbele za haki,
sisi tuliobaki tudumishe amani hii, kama ambavyo wao waliotutangulia hawakujali
dini zao bali taifa hili” alisema Rais Magufuli.
Aliongeza kuwa nchi ya Tanzania imebaki kuwa
kisiwa cha amani, na amani hiyo isichezwe
bali ijengwe na kudumishwa kwa umoja na mshikimamano ili kusaidia
kuitangaza nchi zaidi.
Aidha, viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Rais
wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mheshimiwa Dkt.Ali Mohamedi Shein, Rais
Mstaafu wa Awamu ya Pili Mheshimiwa Alhaji
Ali Hassan Mwinyi, Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa John Samweli Malecela nao wapewa
fursa ya kuzungumza na wananchi kuhusu maadhimisho hayo ya kumbukumbu ya siku
ya Mashujaa.
Viongozi hao, wamesisitiza umuhimu wa kudumisha
amani iliyopo na kusema kuwa ni jukumu la wananchi wote kuhakikisha hawashiriki katika vitendo
vitakavyosababisha uvunjifu wa amani.
Ambapo, waliwataka wananchi kuwaombea Mashujaa
wote waliofariki katika vita mbalimbali wakiwa
katika harakati za kulifanya
Taifa la Tanzania kuwa huru.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim
Majaliwa, alisema kuwa atahakikisha anasimamia utekelezaji wa agizo la Rais la kuitaka
Serikali kuhamia mjini Dodoma.
“Nahamia Dodoma mwezi wa tisa,na nitakapohamia
mawaziri wote lazima wanifuate. Katika hili nitasimamia kwa nguvu zote” alisema
Waziri Mkuu Majaliwa.
Awali, Mheshimiwa Rais Magufuli alisema kuwa
atahakikisha katika kipindi cha utawala wake, Serikali inahamia mjini Dodoma,
kwa vile Rais wa Awamu ya kwanza Mwl. Julius Nyerere alionesha nia ya kufanya
hivyo.
Aliongeza kuwa kwa sasa mji wa
Dodoma unaweza kukidhi mahitaji hayo ya Serikali kwa kutumia miundombinu iliyopo, hata hivyo Serikali
inaendelea kujenga miundombinu mipya.
Maadhimisho ya kumbukumbu za Mashujaa hufanyika Julai
25, ya kila mwaka, kwa kufanya maombolezo ya Mashujaa waliopigana katika vita
mbalimbali katika harakati za kutetea uhuru wa nchi ya Tanzania.
Maadhimisho
ya mwaka huu yamefanyika kwa mara ya kwanza mjini Dodoma, ambapo Rais John
Pombe Magufuli alikuwa mgeni rasmi, ikiwa ni mara yake ya kwanza kuhudhuria
maadhimisho hayo kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
0 comments:
Post a Comment