SERIKALI Mkoa wa Dodoma imesema Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atahamia
rasmi mkoani humo mara baada ya kumalizika kwa vikao vya Bunge
vinavyoanza wiki ijayo, Septemba 6.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana alisema baada ya kufika
Dodoma, ataanza kuratibu utaratibu wa wizara mbalimbali kuhamia katika
Makao Makuu hayo ya nchi.
Pamoja na hayo Jeshi la Polisi limejipanga kuongeza vituo vya Polisi
ili kuimarisha ulinzi wakati serikali itakapohamia na hakuna mwananchi
atakayenyang’anywa ardhi yake kwa sababu yoyote ile.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, Rugimbana alisema
kama mkoa walishauri ujio huo ufanyike mara baada ya kikao cha Bunge na
Waziri Mkuu ameridhia suala hilo.
Alisema Waziri Mkuu atakuwa Mratibu wa wizara zote kuhamia Dodoma na
kazi hiyo ataianza rasmi mara baada ya kuwasili mkoani humo.
Alisema maandalizi yanaendelea vizuri na ukarabati wa nyumba ya Waziri Mkuu umefikia asilimia 90.
Alisema Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Christine Mndeme aliyekutana na makundi mbalimbali kwa ajili ya mapokezi ya Waziri Mkuu.
“Awali tulisema atakuja Septemba Mosi lakini baada ya kushauriana
tumeona aje mara baada ya vikao vya Bunge kwani pilikapilika nyingi
zitakuwa zimepungua, kama serikali ikiamua kuja leo tutaipokea kwani
maandalizi ya serikali kuja Dodoma yamekamilika kwa asilimia 70,”
alisema.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment