Na Adili Mhina, Dodoma.
Tume
ya Mipango imewashauri maofisa wa serikali wenye dhamana ya kusimamia
miradi ya umma kuhakikisha wanatumia mbinu za kisasa katika kuchambua,
kuchagua, kutekeleza na kusimamia miradi ya serikali ili kuhakikisha
malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo yanafikiwa kwa wakati.
Ushauri
huo umetolewa jana mjini Dodoma na Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya
Mipango anayesimamia Klasta ya Miundombinu na Huduma, Mhandisi Happiness
Mgalula alipokutana na maofisa mipango wa Ofisi za Mikoa na
Halmashauri za kanda ya kati iliyojumuisha Mikoa ya Dodoma, Singida na
Manyara kwa lengo la kutoa elimu katika kuandaa, kusimamia, na
kutekeleza miradi ya Umma.
Alisema
kuwa Serikali ilifanya tathmini na kugundua kuwa hakuna vigezo
vinavyofanana katika kuandaa na kuchagua miradi ya umma katika taasisi
mbalimbali za Serikali kitu kinachorudisha nyuma juhudi za kufikia
malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.
“Dira
ya Taifa ya Maendeleo inaelekeza kuwa hadi kufikia mwaka 2025 Tanzania
inatakiwa iwe inchi ya uchumi wa kati na kwa vile tumedhamiria kwa dhati
kifikia hapo ni lazima tujipange upya na kutumia utaalamu wa kisasa na
vigezo vinavyofanana katika kuchagua miradi yenye uwezo wa kulifikisha
taifa huko,” alisema Mgalula.
Kukosekana kwa vigezo vinavyofanana kumesababisha upungufu mkubwa katika miradi ya umma huku ikipelekea miradi mingine kukosa mikopo katika soko la mitaji la ndani au la kimataifa kutokana na kuwa na maandiko yasiyokidhi vigezo vinavyohitajika.
Mgalula
aliongeza kuwa ili kuwekeza katika miradi yenye tija itakayoharakisha
Tanzania kuingia katika nchi za uchumi wa kati, Tume ya Mipango
imedhamiria kuendelea na utaratibu wa kutoa mafunzo kwa walengwa nchi
nzima ili kuongeza utaalam katika kuweka vipaumbele vichache vyenye
ufanisi kwa kila mwaka wa bajeti kuliko kuwa na miradi mingi
isiyokamilika.
Na
kwa upande wa maafisa wanaopata elimu hiyo wanakiri kuwepo kwa
changamoto nyingi katika maandalizi ya miradi ya umma kutokana
kukosekana kwa mfumo unaofanana katika uwekezaji wa miradi ya umma.
“Tayari
tumeanza kuelekezwa namna ya kuandaa miradi kwa kuzingatia vigezo vya
kisasa viliyoainishwa katika mwongozo wa usimamizi wa uwekezaji wa
miradi ya serikali, hii itatusaidia kuwa na utaratibu mmoja na
unaoeleweka tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo kila mradi mpya ulikuwa
na mfumo wake” Alisema Bwana Mkama kutoka Dodoma.
Naye
Afisa Mipango kutoka Halmashauri ya Babati Bw. Godlisten Geofray
alieleza kuwa kuwepo kwa mfumo wa kisasa kutasaidia kuweka kumbukumbu
sahihi za miradi hata ile ambayo haitafanikiwa kupata fedha kwa mwaka
husika pale mfumo wa kanzidata utakapoanzishwa ambao utahifadhi
kubukumbu za miradi yote nchini.
Washiriki
wa mafunzo hayo wameonesha kuridhishwa na juhudi zinazofanywa na Tume
ya Mipango katika kutoa elimu hiyo katika ngazi mbalimbali huku
wakieleza kuwa utaratibu huo utasaidia kuimarisha mawasiliano kwenye
bajeti ya miradi kati ya serikali kuu na serikali za mitaa.
Wataalamu hao wamesisitiziwa kuwa miradi yote itakayohitaji fedha za Serikali katika Bajeti italazimu kufuata utaratibu uliobainishwa katika Mwongozo wa Usimamizi na Utayarishaji wa Miradi ya Uwekezaji katika sekta ya Umma ili kuweza kuimarisha ufanisi na kupata thamani ya fedha.
0 comments:
Post a Comment