Home » » SERIKALI KUWAKAMATA NA KUWAFIKISHA MAHAKAMANI WATU WOTE WALIOSHIRIKI MAUAJI YA WATAFITI-DKT.MWAKYEMBE

SERIKALI KUWAKAMATA NA KUWAFIKISHA MAHAKAMANI WATU WOTE WALIOSHIRIKI MAUAJI YA WATAFITI-DKT.MWAKYEMBE


Na Beatrice Lyimo- MAELEZO


Dar es Salaam.
SERIKALI imesema itahakikisha kuwa wahusika wa mauaji ya Watafiti mkoani Dodoma wanakamatwa na kufikishwa mahakamani ili waweze kujibu mashtaka yanayowakabili.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es salaam na Waziri ya Mambo ya  Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe wakati wa mkutano na  waandishi wa habari juu ya mauaji ya Wataalamu hao yaliyotokea wilayani Chamwino.
Amesema kuwa Serikali imesikitishwa na hatua iliyochukuliwa na  baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Iringa Mvumi wilayani Chamwino kuwaua watafiti hao ambao walikuwa kazini.
Kufuatia hali hiyo amewaagiza Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kushirikiana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) katika kufanya upelelezi wa mauaji ya wataalamu hao  ili wahusika waweze kufikishwa vyombo vya usalama haraka na haki iweze kutendeka.
Amesema kuwa ushirikiano huo utasaidia kuimarisha upepelezi  ambao utawezesha uandaaji wa mashtaka ili wahusika wote waweze kufikishwa Mahakamani kwa ajili ya kujibu mashtaka yanayowakabili.
“Wizara inawataka Mkurugenzi wa Mashtaka DPP ajihusishe kikamilifu na upelelezi wa kesi  hii ya mauaji ya watafiti kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai DCI kwa mujibu wa Sheria ya Huduma ya Uendeshaji  wa Mashtaka” alifafanua Dkt. Mwakyembe.
Ameongeza kuwa ili kukomesha wimbi la wananchi kuchukua sheria mkononi, Wizara itachukua hatua kali kuhakikisha waliohusika kwa namna moja ama nyingine kwa kushawishi, kuhamasisha au kuchochea, kupanga, kushambulia kwa mapanga na kushiriki kuchoma moto gari wanafikishwa mahakamani ili Sheria ichukue mkondo wake.
Katika hatua nyingine, Waziri Mwakyembe amewataka baadhi ya waandishi wa habari kubadilisha mfumo wa kutoa taarifa za matukio zinazochochea uvunjifu wa amani kama vile kuandika kuwa “wananchi wenye hasira kali” maneno ya aina hii hushawishi wengine kufanya hivyo kwa kisingizio cha hasira.
Mbali na hayo Waziri huyo amevitaka vyombo vya dola kuchukua hatua za kisheria kwa wote waliohusika na vitendo vya kuchukua sheria mkononi ikiwemo kuwafikisha mahakamani.

Mwisho


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa