Na: Daudi Manongi-MAELEZO.
NDOTO
ya miaka zaidi ya 40 ya kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu ya Serikali ya
Tanzania imeanza kutimia ndani ya mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya
Tano. Jambo ambalo linastahili kupongezwa na wenye mapenzi mema na nchi
ya Tanzania.
Uamuzi
wa kuhamishia Serikali kutoka jijini Dar es Salaam kwenda Dodoma
limekuwepo tangu mwaka 1973 chini ya chama cha Tanganyika African
National Union (TANU), huku Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma
(CDA) ikiundwa kwa lengo kubwa la kupanga mji, kuishauri na kuisaidia
Serikali ili ihamie huko yalipo makao makuu ya nchi.
Suala hilo, hata hivyo, limesuasua kwa miaka mingi huku jitihada zikionekana kuwa ndogo za kuhamia huko.
Lakini
mwezi Julai mwaka 2016 Rais John Pombe Magufuli ambaye sasa ni
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) alitoa ahadi kuwa atahakikisha
Serikali inahamia Dodoma kabla ya 2020.
Wananchi
kwa ujumla, wakiwemo wasomi na viongozi, wamelipokea tamko la Rais
Magufuli kwa hisia tofauti, ambapo kuna walioliunga mkono kwa bashasha,
wapo waliolipinga, na wengine kufurahishwa na tamko hilo lakini kwa
kuhoji kama linaweza kutimia au la!
Na
kama litatimizwa, bado wanahoji ni njia zipi zitakazofanikisha zoezi
hilo kutokana na ukweli kwamba mara nyingi juhudi hizo zimekuwa
zikikwamishwa na siasa.
Lakini kwa nia njema aliyokuwa nayo Rais wa awamu ya Tano Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli baada ya kutoa tamko hilo Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa alitamka kwamba yeye atahamia Dodoma mwezi
Septemba mwaka huu (2016) huku akiwataka mawaziri wote kumfuata nyuma
baada ya yeye kutangulia.
Walio wengi wamependa tamko hilo na kuliunga mkono suala la kuhamisha wizara zote za serikali kwenda Dodoma sababu kuu ikiwa kutekeleza suala la maendeleo.
Rais Magufuli pia alitoa sababu mbalimbali za kuhamishia Serikali Dodoma ikiwemo kukamilisha ndoto ya Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na pia sababu za kiusalama kwani makao makuu ya nchi yeyote lazima yawe katikati ya nchi na hivyo ni vyema kwa serikali yake kuhamia Dodoma, pia sababu nyingine ni kuipisha Dar es Salaam kuwa mji wa biashara hivyo ni fursa ya kujiandaa kwa hilo.
Aidha Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa aliwasisitiza Mawaziri,Manaibu Waziri,Makatibu wakuu na Manaibu wao kumfuata Dodoma ili kutimiza agizo la Rais Magufuli.
Tayari Mamlaka ya Ustawishaji wa Makao Makuu Dodoma (CDA) ipo na imekuwa ikipangiwa bajeti kila mwaka japo hakuna sheria inayoitambua Dodoma kama mji mkuu lakini serikali inatarajia kuwasilisha muswada wa Sheria wa kuufanya mkoa wa Dodoma kuwa Makao makuu hivi karibuni.
Pia Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akihojiwa kwenye kipindi cha Safari ya Dodoma kinachorushwa na TBC anasema maandalizi ya Ofisi za Serikali Dodoma yamekamilika kwa asilimia 75 na makazi kwa watumishi yamekamilika kwa asilimia 70 hivyo wanaweza kuhamia kwa awamu.
Aidha, Waziri Mkuu Majaliwa amekaribisha wawekezaji kuwekeza katika miradi
mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya ujenzi wa nyumba za watumishi ambao
watajenga nyumba za makazi na kuziuza kwa watumishi wa umma na wananchi.
Amebainisha
kuwa mwekezaji atakayekuwa tayari awasiliane na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Jordan Rugimbana ambaye ndiye anayeratibu shughuli hiyo huku
akikaribisha wawekezaji wa ujenzi wa Hoteli za kitalii na kawaida.
Aidha, Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Bw. Jordan Rugimbana amesema mkoa wake uko tayari kwa asilimia 70 kuipokea Serikali na tayari wamejipanga kwa majengo ya ofisi, makazi na miundombinu mingine.
Umeme,
Maji, Usafirishaji, Makazi na Ofisi vyote vipo vizuri, tumeona sasa
Dodoma iko tayari na Serikali inaweza kuhamia kwa asilimia 70 hadi sasa,
huduma za afya ambapo kuna hospitali yenye huduma nzuri na elimu pia.
Kwa
kweli ni mipango madhubuti ya Rais John Pombe Magufuli ya ndani ya
mwaka mmoja inayofanya utekelezaji huu uwe wenye mafanikio makubwa
nchini.
Waziri
Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa alishatekeleza agizo la Rais Magufuli kwa
kuhamia Dodoma tarehe 30 Septemba 2016 na kupokelewa na viongozi
mbalimbali wa Serikali na wananchi wa mkoa huo. Awamu ya kwanza ya kuhamia Dodoma ilitarajiwa kuanzia
Septemba 2016 mwaka huu hadi Februari, ambapo watakaohamia baada ya
Mheshimiwa waziri mkuu kuhamia ni mawaziri wote,makatibu wakuu wote, na
manaibu katibu wote watahamia, hii ni kwa mujibu wa Mhe. Kassim Majaliwa
“Aidha
kila wizara inatakiwa kuwahamisha watumishi wa idara moja au mbili na
wakati huo huo wakiendelea kuweka utaratibu mwingine wa idara nyingine
kuhamia Dodoma.”
“Awamu
ya pili itakuwa Machi 2017 na Agosti 2017. Kipindi hiki kitawapa fursa
watendaji wa wizara mbalimbali kuweka bajeti zao katika mwaka
wa Fedha wa 2017 18 na kuendelea kuwahamisha watumishi wake kuja
Dodoma. Awamu ya tatu itakuwa kati ya Septemba 2017 na Februari 2018,
ambapo wizara zitaendelea na uhamishaji wa wa watumishi wa idara zilizo
ndani ya wizara zao,” aliongeza Mhe. Majaliwa.
“Awamu
ya nne ni Machi 2018 mpaka Agosti 2018 na awamu ya tano ni Septemba
2018 na Februari 2020. Awamu ya sita ni Machi 2020 na June 2020, itakuwa
ni Ofisi ya Rais ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania watakuwa wanafika
Dodoma.
“Nazishauri Wizara zote katika zoezi hili la kuhamia Dodoma kutumia mifumo ya utunzaji kumbukumbu ya kielektroniki badala
ya kuhama na mafaili yote kutoka Dar mpaka Dodoma kwa kuwa tunataka
Dodoma iwe ya kielektroniki”, anasisitiza Waziri Mkuu.
Hili
ni jambo la kumpongeza Rais Magufuli kwa hatua hii kubwa ambayo imekuwa
katika mipangilio kwa muda sasa imeanza utekelezaji wake ndani ya mwaka
mmoja wa serikali ya Awamu ya Tano. Heko Rais Magufuli kwa kuamua na
kutekeleza, hakika wahenga walisema haja ya mja hunena, muungwana ni
vitendo, Kauli hii imethibitika kwa Kiongozi Mkuu wa Serikali ya Awamu
ya Tano Mzee wa Hapa Kazi Tu.
0 comments:
Post a Comment