Home » » Serikali yajipanga kufungua ubalozi mdogo China

Serikali yajipanga kufungua ubalozi mdogo China

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imejipanga kufungua ofisi ya ubalozi mdogo katika mji wa Guangzhou uliyopo nchini China ili kongeza fursa za kibiashara pamoja na kurahisisha huduma mbalimbali Watanzania wanaoishi nchini humo.

Hayo yamesemwa leo mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Suzan Kolimba alipokuwa akijibu swali la Mhe. Machano Said aliyehoji juu ya kuwekwa kwa ubalozi wa Tanzania nchini China pamoja na utaratibu unaotumika katika kuwapa Visa wananchi ambao wameaamua kuishi nchini humo.

Mhe. Dkt Kolimba amesema kuwa hatua hiyo imefikiwa baada ya Serikali ya China kuchagua majimbo matatu ya Jiangsu, Zhejiang pamoja na Guangdong ili yawe na uhusiano maalum na nchi tatu za Afrika ambapo Tanzania ni moja ya nchi hizo.

“Tunaamini kuwa kwa kufungua ofisi za ubalozi katika mji huu Tanzania itakuwa na fursa ya kuyashawishi makampuni ya mji huo kuja kuwekeza katika nchi yetu pamoja na kutoa huduma mbalimbali kwa Watanzania wanaofanya biashara katika mji huo”, alisema Dkt. Kolimba.

Naibu Waziri huyo ameongeza kuwa mahusiano ya kimataifa ni njia mojawapo ya kuimarisha shughuli za kibiashara na kijamii miongoni mwa wananchi wa nchi hizo mbili katika kuwaletea maendeleo. 

Akiongelea kuhusu Watanzania walioamua kuishi nchini china, Dkt Kolimba amebainisha kuwa utaratibu uliopo sasa kwa wananchi wanaoishi zaidi ya mwaka mmoja katika nchi hiyo wanatakiwa kuwa na kibali cha kuishi nchini humo.

Aidha, Dkt. Kolimba amefafanua kuwa kibali hicho kinapatikana kwa kuwasilisha maombi kwenye wizara inayoshughulika na masuala ya mambo ya ndani ya China na iwapo watakuwa wamekidhi vigezo vinavyotakiwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi hiyo watapatiwa vibali hivyo.   

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa