Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma
Serikali
kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
imejipanga kufungua ofisi ya ubalozi mdogo katika mji wa Guangzhou
uliyopo nchini China ili kongeza fursa za kibiashara pamoja na
kurahisisha huduma mbalimbali Watanzania wanaoishi nchini humo.
Hayo
yamesemwa leo mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Suzan
Kolimba alipokuwa akijibu swali la Mhe. Machano Said aliyehoji juu ya
kuwekwa kwa ubalozi wa Tanzania nchini China pamoja na utaratibu
unaotumika katika kuwapa Visa wananchi ambao wameaamua kuishi nchini
humo.
Mhe.
Dkt Kolimba amesema kuwa hatua hiyo imefikiwa baada ya Serikali ya
China kuchagua majimbo matatu ya Jiangsu, Zhejiang pamoja na Guangdong
ili yawe na uhusiano maalum na nchi tatu za Afrika ambapo Tanzania ni
moja ya nchi hizo.
“Tunaamini
kuwa kwa kufungua ofisi za ubalozi katika mji huu Tanzania itakuwa na
fursa ya kuyashawishi makampuni ya mji huo kuja kuwekeza katika nchi
yetu pamoja na kutoa huduma mbalimbali kwa Watanzania wanaofanya
biashara katika mji huo”, alisema Dkt. Kolimba.
Naibu
Waziri huyo ameongeza kuwa mahusiano ya kimataifa ni njia mojawapo ya
kuimarisha shughuli za kibiashara na kijamii miongoni mwa wananchi wa
nchi hizo mbili katika kuwaletea maendeleo.
Akiongelea
kuhusu Watanzania walioamua kuishi nchini china, Dkt Kolimba
amebainisha kuwa utaratibu uliopo sasa kwa wananchi wanaoishi zaidi ya
mwaka mmoja katika nchi hiyo wanatakiwa kuwa na kibali cha kuishi nchini
humo.
Aidha,
Dkt. Kolimba amefafanua kuwa kibali hicho kinapatikana kwa kuwasilisha
maombi kwenye wizara inayoshughulika na masuala ya mambo ya ndani ya
China na iwapo watakuwa wamekidhi vigezo vinavyotakiwa kwa mujibu wa
sheria na taratibu za nchi hiyo watapatiwa vibali hivyo.
0 comments:
Post a Comment