Home » » Pikipiki Zaleta Mafanikio Katika Sekta ya Elimu

Pikipiki Zaleta Mafanikio Katika Sekta ya Elimu

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na. Lilian Lundo – MAELEZO
Mratibu Elimu Kata (MEK) ni mmoja kati ya kiungo kikubwa kati ya ofisi ya elimu ya wilaya na shule za serikali katika ngazi ya kata ambaye ndiye mfuatiliaji mkubwa wa maendeleo ya elimu ndani ya kata.
Shughuli nyingine zinazofanywa na MEK ni pamoja na kufuatilia maendeleo ya taalamu ya wanafunzi katika kata yake, kukagua ufundishaji wa walimu, kufuatilia mahudhurio ya wanafunzi pamoja na kusimamia vikao mbalimbali vya shule zilizoko katika kata yake.
Asilimia kubwa ya Waratibu Elimu Kata walikuwa wanashindwa kufikia malengo ya kazi zao kutokana na changamoto ya usafiri, ambapo wengi wao walikuwa wakitumia usafiri wa baiskeli ambao ha                                                                                                                                                                                                                                                                      ukuwa usafiri rafiki kutokana na kazi yao ya kukagua shule zote katika kata wanazozisimamia.
Serikali kwa kuliona hilo, kupitia Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania (Education Quality Improvement Programme -Tanzania) EQUIP-T  ilitoa pikipiki kwa kila MEK katika mikoa ya Dodoma, Kigoma, Lindi, Shinyanga, Simiyu na Mara ili kurahisha ufuatiliaji wa mendeleo ya shule zao kwa urahisi.
Pikipiki hizo zimeleta mafanikio makubwa kama  vile kupungua kwa idadi ya wanafunzi watoro, kiwango cha ufaulu kupanda kutokana na ukaguzi wa mara kwa mara wa walimu pamoja na matatizo kutatuliwa kwa haraka kutokana na taarifa za shule kufika wilayani kwa wakati.
Sweetbert Malimi ni Mratibu Elimu Kata wa Sanzawa Wilaya ya Chemba, Mkoani Dodoma anasema kwamba Pikipiki imemuwezesha kushughulikia kwa wakati matatizo yanayotokea katika shule anazozisimamia tofauti na kipindi ambacho hakuwa na pikipiki.
Anaendelea kwa kusema kuwa, matatizo yalipokuwa yakitokea katika shule anazosimamia yalikuwa yakimsubiri MEK hata kwa mwezi mzima. Lakini sasa hivi imekuwa tofauti kutokana na kutembelea shule zake hata mara mbili kwa wiki.
Vilevile ameweza kufuatilia kwa wakati maendeleo ya taaluma ya wanafunzi pamoja na ufundishaji wa walimu ambapo kabla ya kuwa na pikipiki kuna baadhi ya walimu walijisahau kutokana na kutokaguliwa mara kwa mara.
Anaendelea kwa kusema kuwa, ufuatiliaji huo umeletea mafanikio makubwa katika Mkoa wa Dodoma, ambapo ufaulu wa darasa la saba kwa wilaya ya Chemba peke yake ulipanda kutoka asilimia 30 mwaka 2015 mpaka asilimia 46 mwaka 2016. 
Kwa upande wake Mratibu Elimu Kata wa Songambele iliyoko Wilaya ya Kongwa, Mkoani Dodoma amesema kuwa katika kata yake ana shule Sita za kuzifuatilia ambapo kabla ya kupata pikipiki alikuwa anatumia baiskeli kutembelea shule hizo na aliweza kutembelea shule hizo mara moja kwa wiki.
Baada ya kupata pikipiki anauwezo wa kutembelea shule hizo mara tatu hadi nne kwa wiki akifuatilia maandalio ya walimu, maazimio ya kazi, utengenezaji wa zana za kufundishia, mahudhurio ya wanafunzi pamoja na kuhudhuria vikao vya kamati ya shule.
Aidha amesema kuwa, kutokana na ufuatiliaji huo wa mara kwa mara katika shule hizo kumepelekea umakini mkubwa wa ufundishaji wa walimu kwa kufuata taratibu za ufundishaji kama vile kuwa na maandalio, maazimio ya kazi pamoja na kuwa na zana za ufundishaji.
Pia amesema kwamba kwa kutumia pikipiki aliyopewa amekuwa akiwatembelea wazazi ambao watoto wao ni watoro, na kuwashauri juu ya umuhimu wa elimu kwa watoto wao na wazazi wenyewe. Juhudi hizo zimepelekea wazazi wengi kubadilika na kushirikiana na walimu katika kufuatilia mahudhurio na maendeleo ya taaluma ya watoto wao.
Nae, Mratibu Elimu Kata wa Kagera wilaya ya Kigoma Manispaa, Mkoa wa Kigoma  Jovitus Augustus anasema kuwa kabla ya kupewa pikipiki kata yake ilikuwa na changamoto ya utoro kwa wanafunzi pamoja na ufaulu duni wa wanafunzi wa darasa la saba.
“Pikipiki niliyopewa kupitia mpango w EQUIP-T umeniwezesha kutengeneza mipango kazi ya wiki na kuisambaza katika shule zote za kata pamoja na kufuatilia utekelezaji wake,” alifafanua Jovitus.
Aliendelea kwa kusema kuwa pikipiki hiyo imemuwezesha kukagua utekelezaji na utoaji taaluma kwa kukagua maazimio ya kazi na maandilio ya somo pamoja na kufanya vikao vya mara mara kwa mara na walimu ili kupata maelezo ya walimu walioshindwa kutekeleza wajibu wao.
Aidha kupitia juhudi hizo zilizofanyika, ufaulu wa wanafunzi wa darasa la saba shule za msingi za kagera na Mgumile ulipanda pmoja na  mahudhurio ya walimu na wanafunzi katika kata hiyo umeongezeka .
Vilevile umeanzishwa utaratibu wa mitihani ya kata kwa darasa la saba pamoja na kuweka kambi kwa wanafunzi wanaojiandaa na mitihani wa darasa la Saba.
Kwa upande wake mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi ya Mazoezi Bunda iliko Halmashauri ya Mji Bunda Mkoa wa Mara, Mwalimu Vicent Ndunguru, aliipongeza Serikali kupitia Mpango wa EQUIP-T kwa kutoa pikipiki kwa Waratibu Elimu Kata ambao kwa kiasi kikubwa umewarahisishia utendaji kazi wao.
Amesema kuwa, kulikuwa na mambo mengi ambayo yalikuwa hayaendi inavyotakiwa kutokana na MEK anayosimamia shule yake kutotembea shule hiyo mara kwa mara kutokana na ukosefu wa usafiri wa uhakika.
Amesema kuwa, baada ya MEK huyo kupatiwa pikipiki amekuwa akitembelea shuleni hapo mara kwa mara kufuatilia maendeleo ya shule na kuchukua taarifa za shule na kuziwasilisha wilayani kwa wakati.
Mwalimu Ndunguru ambaye pia ni msaidizi wa MEK katika kata ya Nyasura amesema kuwa, MEK huyo amekuwa akiitisha vikao vya mara kwa mara kujadili maendeleo ya shule katika kata yake. Ambapo Shule ya Msingi Mazoezi Bunda ndio eneo lilochaguliwa kwa ajili ya kufanyia mikutano hiyo.
Aliendelea kwa kusema kuwa, MEK huyo amekuwa chachu ya maendeleo ya shule zilizoko katika kata hiyo hasa baada ya kuwa na uhakika na usafiri ambao kwa asilimia kubwa umemuwezesha kufanya kazi zake kwa urahisi na hata kufikia malengo aliyowekewa na mwajiri wake na yale aliyojiwekea yeye mwenyewe katika kuhakikisha ubora wa elimu uaongezeka siku hadi siku kutoka ngazi ya kata mpaka Taifa.
Aidha Mwalimu Ndunguru, ameiomba Serikali kuendeleza na utaratibu wa ugawaji wa pikipiki kwa Waratibu Elimu Kata wa mikoa mingine iliyobaki ili na wao waweze kufanya kazi kwa ufanisi kama ambavyo wenzao waliopewa pikipiki ambavyo wameweza kufanikiwa na hata kupandisha kiwango cha ufaulu na kukomesha tatizo la utoro kwa wanafunzi.
Serikali kupitia mpango huo pia umetoa vishikwambi kwa Waratibu Elimu Kata hao, ambao wamekuwa wakitumia vifaa hivyo kwa ajili ya kupokea taarifa kutoka kwa walimu wakuu wa shule wanazozisimamia na wao kuzituma taarifa hizo ofisi za elimu za wilaya.
Mpango wa EQUIP-T umetoa jumla ya pikipiki 1,000 kwa Waratibu Elimu Kata  wa mikoa ya Dodoma, Kigoma, Lindi,  Shinyanga, Simiyu, Shinyanga na Mara. Pikipiki hizo zilitolewa kati ya mwaka 2014 na 2015 ambapo mpango huo unawawezesha waratibu hao kupata fedha ya mafuta na utengenezaji wa pikipiki hizo kila mwezi.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa