Home » » SERA YA MAENDELEO YA MICHEZO YA MWAKA 1995 YAFANYIWA MAREKEBISHO KUENDANA NA MAHITAJI YA SASA.

SERA YA MAENDELEO YA MICHEZO YA MWAKA 1995 YAFANYIWA MAREKEBISHO KUENDANA NA MAHITAJI YA SASA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na Daudi Manongi,MAELEZO,DODOMA.

Serikali kupitia Wizara ya Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo imesema kuwa inakamilisha mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 ili kuhakikisha inaendana na mahitaji ya sasa katika maendeleo ya michezo nchini.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Anastazia Wambura wakati akijibu swali la Mbunge wa Mafinga Mjini Mhe.Cosato Chumi aliyetaka kujua mipango ya Serikali katika kufufua mchezo wa Riadha Bungeni Mjini Dodoma leo.

“Serikali kwa kushirikiana na wadau inatekeleza programu mbalimbali za kuendeleza  mchezo wa riadha nchini ikiwemo Kilimanjaro Marathon,Bagamoyo Marathon,Heart Marathon na Tulia Marathon ambayo hushirikisha wanariadha kutoka nje”,Aliongeza Mhe.Wambura.
Aidha pamoja na hayo Mhe.Wambura amesema kuwa Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia  pamoja na Ofisi ya Rais TAMISEMI imeendesha mashindano ya UMISETA na UMITASHUMTA  ambayo pamoja na mambo mengine yanalenga kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana wetu katika mchezo wa riadha.

Akizungumzia suala la miongozo ya Kiserikali amesema kuwa Wizara yake inakamilisha taratibu za kuandaa miongozo ya kiserikali ili kuwezesha wadau wote kuendesha  shughuli  zao katika mazingira ya weledi na stadi bora za michezo.

Hata hivyo Naibu Waziri uyo amesema kuwa nchi yetu imeanza kufanya vizuri katika mashindano ya Riadha kama ilivyokuwa katika miaka ya nyuma kupitia kwa wanariadha wake kama Francis Naal,Samson Ramadhani,Gidamis Shahanga,Juma Ikangaa,Suleiman Nyambui na Filbert bayi na hivyo kuitangaza nchi yetu.

“Nchi yetu kwa sasa imeanza kupata mafanikio katika riadha kupitia wanariadha wetu kama Alphonce Simbu aliyeshinda medali ya dhahabu kwenye mashindano ya standard Chartered Mumbai Marathon,Cecilia Ginoka Panga aliyeshinda Beijing International Half Marathon na Giniki Gisamoda aliyeshinda Shanghai International Half Marathon,wote hawa wanaitangaza nchi yetu vizuri na kuifanya ifahamike na hivyo kuvutia watalii ”Alisisitiza Mhe.Wambura.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa