Home » » MWIJAGE AVIFUTIA UMILIKI VIWANDA 10

MWIJAGE AVIFUTIA UMILIKI VIWANDA 10

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Magnus Mahenge, Dodoma.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Charles Mwijage.
SERIKALI imetangaza kuwa viwanda 10 vilivyokuwa vimeshindwa kuzalisha au kuendelezwa, vimefutiwa umiliki wake na kupewa wawekezaji wengine kuvifufua. Aidha, viwanda 11 kati ya 56 vilivyokuwa vimefungwa, vimefufuliwa vitaanza uzalishaji wake wakati wowote.
Akizungumza mjini Dodoma jana, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alitaja viwanda 10 ambavyo wamepewa wamiliki wengine kutokana na umiliki wa awali kufutwa kuwa ni Kiwanda cha Mkata Saw Mills, Kiwanda cha Korosho Lindi na Kiwanda cha Taifa cha Chuma na Manawa Ginnery.
“Kiwanda cha Tembo Chipboard, Mang’ula Mechanical Tools, Mgodi wa Pugu Kaolin, Dabaga Tea Factory, Kiwanda cha Polysack na Kiwanda cha Kilimanjaro Textile Mills cha Arusha,” alivitaja Mwijage ikiwa ni siku chache baada ya kubanwa na Rais John Magufuli kuchukua hatua dhidi ya wawekezaji walioshindwa kuendeleza viwanda miaka 20 tangu serikali ilipovibinafsisha.
Alivitaja viwanda vitano kati ya 11 ambavyo wamiliki wengine wamepewa kuvifufua ni Kiwanda cha Mvinyo Dodoma (DOWICO), Kiwanda cha Mafuta Morogoro (MOPROCO), Tabora Textile Mills, Manonga Ginnery na kilichokuwa Kiwanda cha Viatu Morogoro.
Katika orodha hiyo, pia alivitaja viwanda vinne ambavyo vinafufuliwa na wawekezaji wapya baada ya wawekezaji wa awali kutovifufua ni Morogoro Canvas Mills (TSSA), Mwanza Textile Mills (TSSA), Kiwanda cha Nguo cha Urafiki (TSSA) na Kiwanda cha Mutex (LAPF).
Mwijage alitaja viwanda viwili vinakusudia kufufuliwa na tayari mipango ya uwekezaji, imewasilishwa na vipo katika uangalizi wa miezi mitatu kuanzia Agosti 10, mwaka huu ni pamoja na Kiwanda cha Korosho Kibaha na Newala I Cashewnuts Factory.
Alisema viwanda vitano vipo katika uangalizi hadi Agosti 22, mwaka huu, ambapo serikali itachukua hatua dhidi yake kuanzia wakati huo ambavyo ni Sabuni industries Limited, Tanzania Moshi Pesticides, Tanzania Bag Corporation, Ilemela Fish Processing Plant na Mzizima Maize Mill.
Mwijage alisema ubinafsishaji nchini, ulihusisha viwanda, mashamba, kampuni za biashara, hoteli na kampuni za usafirishaji zipatazo 431, na kati yake, viwanda vilikuwa 156 ambavyo 62 vinafanya kazi vizuri, 28 vinafanya kazi kwa kusuasua na viwanda 10 vilibinafsishwa kwa kuuzwa mali moja kwa moja.
Alisema katika orodha hiyo, Kiwanda cha Mwanza Tanneries ambacho hakijaendelezwa tangu kubinafsishwa miaka ya 1990, mwekezaji wake ameamua kukirudisha serikalini.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa