Home » » SERIKALI KUNUNUA MASHINE ZA DNA KWENYE MAABARA ZA KANDA

SERIKALI KUNUNUA MASHINE ZA DNA KWENYE MAABARA ZA KANDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na Beatrice Lyimo-MAELEZO, DODOMA

Serikali imedhamiria kununua mashine tatu za vipimo vya vinasaba (DNA) ili zitumike katika maabara za Kanda na hivyo kusogeza huduma karibu na wananchi.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeo ya Jamii, Jinsi, Wazee na Watoto Dkt. Hamis Kigwangala wakati akijibu swali la Mbunge wa Chumbuni Mhe. Ussy Pondeza kuhusu ucheleweshwaji wa matokeo ya uchunguzi wa sampuli ikiwemo sampuli za makosa ya jinai.

Dkt Kigwangala amesema kuwa Serikali ina mkakati wa kuongeza mashine hizo ili kuwezesha uchunguzi kufanyika kwa wakati kwa vielelezo vya makosa ya jinai ikiwa ni pamoja na vitendo vya udhalilishaji kwa wanawake na watoto.

" Sampuli za uhalali wa watoto kwa wazazi zinafanyika kwa wepesi zaidi kuliko sampuli za makosa ya jinai kwani sampuli hizo zinachukuliwa moja kwa moja toka kwa wahusika hivyo kurahisisha uchunguzi wake endapo wahusika wa uchukuaji watachukua kwa umahiri na uhifadhi utafanyika kwa namna stahili" amefafanua Dkt. Kigwangala.

Aidha, Dkt. Kigwangala amesema kuwa sampuli za uchunguzi wa makosa ya jinai zinachukuliwa toka maeneo ya matukio hivyo uchunguzi wake unaweza kuchukua muda zaidi kutegemeana na aina ya sampuli na eneo zilipotoka.

Vilevile Dkt. kigwangala aliongeza kuwa Serikali inampango wa kuanzisha kituo cha kupima vinasaba (DNA) Mkoani Mbeya kwa lengo la kupunguza ucheleweshaji wa matokeo ya uchunguzi.

Mbali na hayo akijibu swali la Mbunge wa Mtwara Vijijini Mhe. Hawa Ghasia kuhusu Serikali kuagiza tohara kuwa lazima kwa wanaume nchini, Dkt. kigwangala amesema kuwa si rahisi kwa Serikali kuagiza tohara  kuwa lazima japo kuwa inafaida kiafya kwa wananchi.

" Tohara inasaidia kupunguza maambukizi ya Saratani ya shingo ya Uzazi kwa wanawake pamoja na maambukizi ya virusi vya Ukimwi" ameongeza Dkt. kigwangala.

Aidha, amesema kuwa elimu kuhusu tohara imefikishwa kwa wananchi kwa kiasi kikubwa ambapo Serikali kwa kushirikiana na wadau katika Mikoa ya kipaumbele  imekuwa ikitoa elimu kabla na baada ya huduma ya tohara katika vituo vya kutolea huduma za afya.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa