Home » » NAIBU WAZIRI BITEKO ATOA CHANGAMOTO CHUO CHA MADINI

NAIBU WAZIRI BITEKO ATOA CHANGAMOTO CHUO CHA MADINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Naibu Waziri mpya wa Madini Dotto Biteko akizungumza na wafanyakazi wa Chuo cha Madini kilichopo Dodoma, (hawapo pichani) alipowatembelea Januari 15 mwaka huu.
Mkutubi Msaidizi wa Chuo cha Madini (MRI), Rachel Lugoye (kulia) akimweleza Naibu Waziri wa Madini Dotto Biteko na Ujumbe wake (kulia) utendaji kazi wa Maabara katika Chuo hicho, wakati wa ziara ya Naibu Waziri Januari 15 mwaka huu.
Mhandisi Mchenjuaji wa Chuo cha Madini (MRI), Dkt. Abdulrahman Mwanga, akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko na Ujumbe wake kuhusu mitambo mbalimbali iliyo katika maabara za Chuo inavyofanya kazi, wakati wa ziara ya Naibu Waziri kujionea utendaji kazi wao, Januari 15 mwaka huu.
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa Chuo cha Madini (MRI) kilichopo Dodoma, alipowatembelea hivi karibuni.

Na Veronica Simba – Dodoma
Naibu Waziri mpya wa Madini Dotto Biteko ametembelea Chuo cha Madini (MRI) na kutoa changamoto kadhaa kwa Menejimenti na wafanyakazi wote, ili kiwe na tija stahiki kwa Taifa.
Akizungumza baada ya kutembelea sehemu mbalimbali za Chuo hicho kilichopo Dodoma, Januari 15 mwaka huu, Naibu Waziri alieleza kutokuridhishwa kwake na utekelezaji hafifu wa masuala kadhaa muhimu na hivyo kutoa changamoto kwa uongozi wa Chuo kuyafanyia kazi mapema.
Moja ya mambo muhimu aliyoelekeza yatekelezwe ni pamoja na matumizi mazuri ya rasilimali za Serikali kwa manufaa ya Taifa. Aliwataka kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais John Magufuli anayetaka rasilimali kidogo inayopatikana nchini itumike vizuri na kuleta matokeo.
“Mathalani, viko vifaa vya mamilioni ya shilingi katika baadhi ya maabara zenu na havijawahi kufanya kazi kwa muda wa miezi Sita sasa. Vinachakaa na kuharibika tu. Akija aliyetufadhili kununua vile vifaa, atatushangaa. Tutaonekana wote hatuna uwezo wa kufikiri kumbe ni watu wachache tu wanaosababisha,”alisema.
Kufuatia suala hilo, Naibu Waziri aliagiza maabara zote zenye vifaa ambavyo havifanyi kazi zirekebishwe na zianze kufanya kazi kufikia mwisho wa mwezi huu wa kwanza.
Changamoto nyingine aliyoitoa Naibu Waziri ni kwa Chuo kufanya tafiti ili kuisaidia Serikali kujua mahitaji halisi ya rasilimali watu kwenye sekta ya madini.
“Ninyi ni tofauti kabisa na taasisi nyingine zinazofanya biashara. Mkifanya vizuri, maafisa wetu wa madini kule mikoani na kwingineko kwenye kanda watafanya kazi rahisi sana. Kwa sababu ninyi mtakuwa mmeshafanya utafiti kwa niaba ya Wizara kugundua mahitaji ya rasilimali watu kwenye sekta ya madini.”
Akifafanua zaidi, alisema kwamba Wizara inategemea kupata chemchemi ya fikra kutoka kwenye taasisi hiyo ya Chuo. Alisema, Chuo kinatarajiwa kuzalisha wataalam wazuri ambao watakwenda kufanya kazi sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kwenda kufundisha wachimbaji wadogowadogo namna nzuri ya kuchenjua madini kwa kuzingatia usalama wa mazingira na kupata tija ili kupandisha hadhi ya mavuno ya rasilimali wanayopata.
Aidha, aliongeza kuwa haipendezi kuona Chuo kikifundisha vijana wengi wa kitanzania lakini kwenye migodi kunakuwa na wafanyakazi wa kigeni wakifanya kazi ambazo watanzania wanaweza kufanya.
“Changamoto kwenu kama Chuo, je, vijana wetu mnawanoa kiasi cha kutosha kushindana katika soko la ajira? Ninyi ni taasisi ya kitaaluma, mnatakiwa kuyaona mambo ya kesho leo. Na mambo ya jana yawasaidie kuboresha kesho ya nchi hii.”
Vilevile, aliwataka kuachana na utamaduni wa kulalamika kwa masuala mbalimbali badala yake wahakikishe wanatimiza wajibu wao ipasavyo na matokeo ya kazi yao yaonekane. Alisema, matokeo mazuri ya kazi ndiyo yatakayoihamasisha Serikali kuona umuhimu wa kuboresha yale wanayoyalalamikia ikiwemo suala la maslahi.
Hii ni ziara ya kwanza ya Naibu Waziri Biteko katika Chuo cha Madini tangu alipoteuliwa kushika nafasi hiyo na kuapishwa na Rais John Magufuli Januari 8 mwaka huu, Ikulu jijini Dar es Salaam.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa