Home » » BAJETI YA MWAKYEMBE YATIKISA BUNGE,YAPITA

BAJETI YA MWAKYEMBE YATIKISA BUNGE,YAPITA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, akijibu hoja za wabunge waliochangia mjadala wa kupitisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2014/15 bungeni Dodoma, jana.  

Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe jana usiku alikuwa katika wakati mgumu wakati Bunge lilipoketi kama Kamati ya Matumizi, kiasi cha kutishia bajeti ya wizara yake kukwama.
Hata hivyo, Makadirio ya Mapato na Matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2014/15 yalipitishwa.
Wabunge wa vyama vyote walimbana Dk Mwakyembe na kutoa shilingi karibu katika kila kifungu wakihoji mambo mbalimbali hasa juu ya mgogoro wa umiliki wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (Uda), uimarishaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATC), usafiri wa majini hususan usalama wa meli ya Mv Victoria.
Sakata la Uda
Sakata hilo la Uda lilisababisha mvutano baina ya Naibu Spika, Job Ndugai na Dk Mwakyembe ambaye alilalamikia mjadala wa Uda kuruhusiwa katika hotuba ya wizara yake.
Hata hivyo, Ndugai alipangua hoja hiyo akisema mbali na kwamba Uda inagusa wizara nyingi, lakini ni suala linalohusu uchukuzi hivyo ilikuwa sahihi kujadiliwa katika mjadala huo.
Mbunge wa Nzega (CCM), Dk Hamisi Kigwangalla ndiye aliyeibua suala hilo kwa kuhoji sababu ya Serikali kutoa taarifa zinazokanganya kuhusu Uda, hali kamati anayoiongoza ilishakaa na pande zote husika wakiwamo wataalamu na kuwa na hitimisho kwamba Kampuni ya Simon Group Ltd ni waendeshaji halali wa shirika hilo.
Hoja hiyo iliibua mjadala ambao pia ulichangiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Peter Serukamba ambaye alisema Simon Group Ltd waliuziwa kihalali hisa za Uda na kwamba wamiliki hao wanazongwa kutokana na kwamba ni ngozi nyeusi (Watanzania).
Kwa upande wake, Waziri Kivuli wa Uchukuzi, Moses Machali alisema maelezo ya Serikali kuhusu umiliki wa Uda yana mkanganyiko, hivyo Simon Group Ltd wanaandamwa bila sababu za msingi.
Kwa upande wake Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema Serikali inajiweka uchi, kutokana na majibu yanayokinzana kutoka kwa mawaziri na Kamati za Bunge.
Hoja ya Mbowe ilipingwa na waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), aliyesema Serikali haijajivua nguo na kwamba itachukua hatua za kuliweka sawa kwa kutoa taarifa moja.
Awali, akihitimisha hotuba yake huku akipangua hoja mbalimbali za wabunge, Dk Mwakyembe alisema mwaka 2012/2013 ilikuwa ni kuitoa Sekta ya Uchukuzi kutoka katika chumba cha wagonjwa mahututi.
Kambi ya Upinzani
Mapema akisoma hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, Machali alisema Mei 15 mwaka huu, Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima aliliambia Bunge kuwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ilikuwa na hisa asilimia 51 na Serikali 49.
Alisema mara baada ya kutolewa taarifa hiyo, Mkurugenzi wa Simon Group, Robert Kisena alidai kuwa kampuni hiyo inamiliki asilimia 76.79 na Serikali asimilia 23.26 tu.
“Je, ni nani mwongo kati ya Serikali na Simon Group? Je, aliye mwongo kati yao ndani na nje ya Bunge anachukuliwa hatua gani?” alihoji.
Masuala mengine ambayo yaliibua mjadala wakati Bunge lilipokaa kama Kamati ya Matumizi ni kuhusu Shirika la Ndege la ATCL, Upanuzi wa Viwanja vya Ndege vya Mwanza na Kilimanjaro (Kia) na usalama wa Meli ya Mv Victoria.
Majibu ya Dk Mwakyembe
Akijibu hoja hizo, Dk Mwakyembe alisema bajeti ya mwaka huu wa fedha 2014/2015 ni ya kuiendeleza sekta ya uchukuzi ili iweze kukimbia.
“Mwaka 2013/2014 ilikuwa ni bajeti ya kuifanya sekta hii ya uchukuzi ianze kutembea. Nawahakikishia mwaka wa fedha wa 2014/2015 kutakuwa na manchibadiliko makubwa katika sekta ya reli itaanza kukimbia,” alisema.
Alisema kwa mara ya kwanza nchi itakuwa na vichwa vya treni 51 vya uhakika tofauti na idadi ya sasa ambayo ni vichwa vinane tu vya kusuasua na kwamba kwa kuwa na vichwa hivyo kutawezesha kusafirisha tani milioni 1.5 za mizigo kulinganisha na tani 200,000 za sasa.
Kuhusu wabunge, mawaziri na wafanyakazi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kutumia fedha nyingi kwa ajili ya safari, Dk Mwakyembe alisema taarifa hiyo si sahihi na kwamba hakuwahi kufanya safari yoyote ya mafunzo kwa sababu taaluma yake.
Kwa upande wa ATCL, Dk. Mwakyembe alisema deni la Sh133 bilioni ndilo linalowasumbua na kwamba Serikali inahangaika kulichukua.
Awali, Kambi rasmi ya upinzani Bungeni, iliilipua Wizara ya Uchukuzi kwa kile ilichodai ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka ikiwemo kuhoji hatua ya wizara hiyo kujitengea Sh1.1 bilioni kwa ajili ya kulipana posho na chai.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa