Home » » HAMAD RASHIDI ;NITAGOMBEA URAIS 2015

HAMAD RASHIDI ;NITAGOMBEA URAIS 2015

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mjumbe wa Bunge la Katiba, Hamad Rashid Mohamed akichangia hoja katika kikao cha bunge hilo, mjini Dodoma Aprili 22 mwaka huu. Picha na Maktaba  

Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed amesema anapanga kujitosa kwenye kinyang’anyiro cha urais katika Uchaguzi Mkuu mwakani.
Akizungumza katika mahojiano maalumu hivi karibuni mjini Dodoma, Hamad Rashid alisema: “Kama Mwenyezi Mungu akinijalia uhai na uzima mwakani, ninatarajia kuingia kwenye kinyang’anyiro cha urais ama wa Muungano au wa Zanzibar.
“Ila sijaamua kama ni Bara au Zanzibar; kama ni chama cha CUF au kingine, hayo yote yatakuja baadaye,” alisema Hamad Rashid.
Mohamed ambaye ana mgogoro mahakamani na chama chake cha CUF, ametoa kauli hiyo wakati tayari viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), CUF kikiwamo wanajipanga kusimamisha mgombea mmoja wa urais katika uchaguzi ujao.
Mbali na CUF, vyama vingine vinavyounda Ukawa ni NCCR-Mageuzi na Chadema ambavyo pia vinakusudia kusimamisha mgombea mmoja kwa nafasi za ubunge na udiwani, lengo likiwa kukabiliana na nguvu ya chama tawala, CCM.
Hamad Rashid aliyekuwa Mjumbe wa Baraza Kuu CUF, alifutwa uanachama Januari 4, 2012 na Baraza la Uongozi la chama hicho kwa madai ya kukihujumu kwa mujibu wa kifungu 63 (1) (j) na 64 (1-5) cha Katiba ya CUF. Wengine waliotimuliwa pamoja na Hamad ni Doyo Hassan Doyo, Shoka Hamis Juma na Juma Said Sanani.
Sakata la Hamad kuvuliwa uanachama lilianza baada ya kutangaza kuwania nafasi ya Katibu Mkuu wa chama hicho katika uchaguzi wa mwaka huu, nafasi inayoshikiliwa na Seif Shariff Hamad ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar.
Hata hivyo, Januari 10, 2012 Hamad Rashid na wenzake waliiomba Mahakama iwatie hatiani wadhamini wa CUF, kwa kukiuka amri ya Mahakama kutokana na uamuzi wa Baraza la Taifa la Uongozi la chama hicho kuwafukuza uanachama wakiwa tayari wameweka zuio.
Baadaye Septemba mwaka jana, Hamad alikaririwa na gazeti moja akisema suluhu yake na CUF haiwezi kupatikana kwa kuwa kuna baadhi ya mambo ambayo hakubaliani nayo ndani ya chama hicho.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa