MBUNGE wa Viti Maalumu, Susan Lyimo (Chadema) amebanwa kuthibitisha
kauli yake aliyoitoa bungeni kuwa serikali ilinunua magari ya Polisi
‘Washawasha” 777 wakati ilitumia 50 pekee wakati wa Uchaguzi Mkuu
uliopita.
Mbunge huyo alitakiwa kuthibitisha hilo na Mwenyekiti wa Bunge, Mussa
Azzan Zungu kwa kupeleka uthibitisho au kufuta kauli yake baada ya
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yussuf Massauni kuomba
mwongozo kupitia kanuni ya 64(a) na 63(1) akiomba mwongozo wa hatua gani
anaweza kuchukuliwa Lyimo.
“Kanuni zipo, zinampa haki kila mbunge na Naibu Waziri ameomba
mwongozo kwa kanuni ya 64(a) na 63(1) sasa kwa kuwa Susan hayupo hapa
sasa hivi, akirejea jioni mwongozo wangu ni kwamba afute maneno yake au
alete uthibitisho,” alisema Mwenyekiti huyo wa Bunge.
Lyimo katika mchango wake kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto, alisema serikali imenunua magari ya
‘Washawasha” 777 mwaka jana wakati wa Uchaguzi Mkuu lakini yaliyotumika
ni 50 pekee.
0 comments:
Post a Comment