Home » » Serikali kushirikiana na Sekta Binafsi katika kuongeza uzalishaji wa mbegu za mazao ya mafuta.

Serikali kushirikiana na Sekta Binafsi katika kuongeza uzalishaji wa mbegu za mazao ya mafuta.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.

SERIKALI kwa kushirikiana na na Sekta Binafsi nchini imeandaa mikakati inayolenga kuongeza tija na uzalishaji wa mbegu za mazao ya mafuta hususan zao la alizeti ambao uzalishaji wake umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka.

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe. Tate William Ole-Nasha wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Jesca Kishoa kuhusu Serikali kuweka msukumo kwa mazao ya mafuta katika mikoa husika kwa faida ya nchini na wakazi wa mikoa hiyo.

Mhe. Ole-Nasha amesema kwamba, Taifa limekuwa likitumia fedha nyingi za kigeni katika kuagiza mafuta ya kula wakati kuna vyanzo vingi vya mafuta ikiwemo alizeti na michikichi, hivyo ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali inashrikiana na Sekta Binafsi kuweka mikakati itayolenga kuongeza tija na uzalishaji wa mbegu za mazao ya mafuta hususani alizeti.

Amesema kuwa, katika mkoa wa Singida vikundi mbalimbali vimeundwa na taasisi mbalimbali za Serikali na zile zisizo za Kiserikali ambapo moja ya malengo ya vikundi hivyo ni kuongeza thamani ya zao la alizeti na upatikanaji wa pembejeo ili kukuza tija na uhakika wa soko kwa wakulima.

“Kigoma ni mkoa pekee nchini unaolima zao la michikichi kwa kiwangho kikubwa ikilinganishwa na maeneo mengine nchini”, alisema Ole-Nasha.

Ameongeza kuwa, Hadi sasa mkoa una zaidi ya hekta 18,924 za michikichi zenye tija ya tani 1.6 kwa hekta, uzalishaji huo bado ni mdogo ikilinganishwa na tani 4 kwa hekta zinazoweza kuzalishwa.

Amesema pia ili kuongeza tija, mkoa kupitia Halmashauri zake unaendelea kuhamasisha wananchi kufufua mashamba ya zamani ya michikichi kwa kuyapalilia, kuondoa majani yaliyozeeka na kuanzisha mashamba mapya yatakayokuwa yanapandwa mbegu bora.

“Mkoa kwa kushirikiana na wadau wengine umeshaanza kuzalisha miche bora ya michikichi ambayo itasambazwa kwa wakulima kwa gharama nafuu ili kila mkulima apande miche 137 inayotosha hekta moja", aliongeza Ole-Nasha.

Ametoa wito kuwa, Serikali Kuu na ya Mkoa zinakaribisha wawekezaji zaidi kuwekeza katika uzalishaji mkubwa na viwanda vya kati na vikubwa vya kukamua mafuta na bidhaa nyingine zitokanazo na michikichi.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa