Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.
SERIKALI
kupitia Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji inashauriana na
Wawekezaji wa Viwanda vinavyofanya kazi kwa kusuasua pamoja na vile
vilivyofungwa ili kuviwezesha viwanda hivyo kufanya kazi.
Kauli
hiyo imetolewa leo Bungeni mjini Dodoma na Waziri wa Viwanda, Biashara
na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage wakati akijibu swali la Mbunge wa
Viti Maalum, Mhe. Savelina Mwijage ambaye alitaka kujua Serikali ina
mpango gani wa kuviboresha viwanda vya kizamani ili viweze kufanya kazi
vizuri kwa faida ya nchi.
Mhe.
Mwijage amesema kuwa, viwanda vingi vinavyotumia teknolojia ya zamani
ambavyo havifanyi kazi au kuzalisha kwa kusuasua ni vile
vilivyobinafsishwa ambapo katika tathmini iliyofanywa na Wizara hiyo kwa
kushirikiana na Ofisi ya Msajili wa Hazina inaonyesha kuwa kati ya
viwanda vilivyobinafsishwa, viwanda 24 vinafanya kazi kwa kusuasua na
viwanda 37 vimefungwa kote nchini.
Aidha,
katika mkoa wa Kagera, Kiwanda cha NMC Old Rice Mill kimefungwa wakati
kiwanda cha Kagera Tea Co. Ltd (MARUKU) kinafanya kazi kwa kusuasua.
“Kusuasua
kwa kiwanda hiki na vingine vyote nchini kunatokana na uchakavu wa
mitambo katika baadhi ya Viwanda, ushindani katika soko, kupungua kwa
mtaji na kutopatikana kwa malighafi”, alisema Mhe, Mwijage.
Ameongeza
kuwa, Serikali inafanya majadilaino na wawekezaji wa viwanda
vinavyofanya kazi kwa kusuasua pamoja na vile vilivyofungwa ili
kuviwezesha viwanda hivyo kufanya kazi tena ambapo katika majadiliano
hayo yanayoendelea, yanahimiza matumizi ya ya teknolojia ya kisasa
katika uzalishaji viwandani.
“Tunawashauri
wawekezaji walioshindwa kuendesha ipasavyo viwanda vyao kuingia ubia na
wawekezaji wengine wenye uwezo wa kuviendesha kwa tija ili tuongeze
ajira, tuzalishe bidhaa kwa ajili ya soko la ndani na nje na kulipa
kodi”, alisema Mhe. Mwijage.
Amesisitiza
kuwa, Wizara yake kwa kushirikiana na Mamlaka nyingine itaendelea
kulinda viwanda vya ndani kwa kuhakikisha bidhaa zote ziingiazo
zinakidhi viwango na zinatozwa tozo stahiki.
0 comments:
Post a Comment