Naibu
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Wenye Ulemavu) Mhe.Dkt.Abdallah Possi
akichukua dondoo za Mkutano wa 9 wa nchi ambazo zimeridhia Mkataba wa
Haki za Watu Wenye Ulemavu uliofanyika katika Ukumbi wa Umoja wa Mataifa
Marekani tarehe 15 Juni, 2016.
WAZIRI POSSI AIWAKILISHA VYEMA AFRIKA MKUTANO WA UMOJA WA MATAIFA WA KUTOKOMEZA UMASIKINI NA KULETA USAWA KWA WATU WENYE ULEMAVU
Na.MWANDISHI WETU
Siku ya tarehe 15
Juni, 2016, Mhe. Dkt. Abdallah Possi (MB), Naibu Waziri, Ofisi ya
Waziri Mkuu alishiriki katika Mjadala wa kutokomeza umasikini na
kuleta usawa kwa watu wenye ulemavu. Majadiliano hayo yalikuwa ni moja
ya mikutano muhimu iliyolifanyika katika Mkutano wa 9 wa nchi ambazo
zimeridhia Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu uliofanyika New York,
Marekani.
Mwenyekiti wa
majadiliano hayo alikuwa ni Bi. Ellen Maduhu, Afisa katika ofisi ya
uwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ambaye pia ni
Makamu wa Raisi wa Kamati ya Mkutano wa Nchi ambazo zimeridhia Mkataba
wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (Vice President of the Conference of State
Parties to the Convention on the Rights of Persons of Disabilities)
Mhe. Dkt. Possi
alikuwa ni mmoja wa watoa mada aliyeliwakilisha bara la Afrika. Katika
majadiliano hayo kulikuwa na watoa mada wengine watano kutoka mataifa
mengine wakiwemo Ms. Asa Regner, Waziri wa watoto, wazee na usawa wa
kijinsia kutoka Sweden; Bw. Joelson Dias, mjumbe wa Kamati maalumu
inayoshughulikia haki za watu wenye ulemavu, Brazil; Bi. Silvia
Quan kutoka Taasisi ya Haki za Binadamu wakiwemo watu wenye ulemavu,
Brazil; Ms. Mercedes Juan, kutoka Kamisheni ya Taifa kwa ajili ya
maendeleo na ujumuishwaji wa wenye ulemavu, Mexico; na Bi. Emi Aizawa
kutoka Taasisi ya Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA)
Katika Majadiliano hayo, watoa mada walilenga hoja zao katika kujibu maswali ya mambo makuu matatu.
Jambo la kwanza
lilikuwa kuelewa hatua zilizochukuliwa na nchi husika na wadau wengine
kupunguza umaskini na kukosekana kwa usawa kwa watu wenye ulemavu.
Jambo la pili
lilikuwa kujua hatua zilizochukuliwa na nchi husika na wadau wengine
katika kuhakikisha masuala muhimu ya watu wenye ulemavu yanaingizwa
katika sera zao za kitaifa za maendeleo na mipango ya kuondoa umasikini
na kuhakikisha usawa katika jamii.
Suala la tatu
lilikuwa kuelewa hatua zilizochukuliwa na wadau mbalimbali katika
kuhakikisha kwamba mipango ya maendeleo endelevu ya ajenda 2030
yanajumuisha masuala muhimu ya kuwakomboa watu wenye ulemavu kwa
kuwaletea maendeleo na usawa.
Katika mada yake,
Mhe. Dkt. Possi alieleza kuwa katika kuhakikisha Tanzania inatoa haki
na usawa kwa watu wenye ulumavu, Serikali imetengeneza sheria, sera na
miongozo mizuri ya kusimamia usawa miongoni mwa watu wenye ulemavu.
Alibainisha kuwa
sera na Sheria nzuri zilizopo zinakabiliwa na changamoto mbali mbali
katika utekelezaji wake ikiwa ni pamoja na changamoto za kiuchumi. Hata
hivyo, Serikali imejipanga kukabiliana na changamoto hizo.
Vile vile Mhe.
Possi alieza kuwa uchumi duni katika nchi nyingi zinazoendelea umekuwa
chanzo kikubwa cha kudhoofisha jitihada za kuleta maisha bora kwa watu
wenye ulemavu.
"Tanzania, kama
mataifa mengine yanayoendelea, inakabiliwa na changamoto za kiuchumi
ambazo zinaathiri maisha ya watu wenye ulemavu, kama vile upatikanaji wa
maji safi, chakula, afya na elimu. Pia kuna tatizo la jumla la ukosefu
wa ajira, ambayo pia huathiri watu wenye ulemavu", alieleza Mhe. Possi.
Dkt. Possi pia
aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa mitazamo hasi ya kijamii, na
ukosefu wa vifaa muhumu vya kuwasaidia watu wenye ulemavu (assistive devices)
vinachangia kwa kiasi kikubwa kwa watu wenye ulemavu kutoshirikishwa
katika masuala ya jamii ikiwa ni pamoja na shughuli za kiuchumi.
Tatizo la
upatikanaji wa vifaa kwa watu wenye ulemavu limekwamisha maendeleo na
ustawi bora wa watu wenye ulemavu hapa nchini, hususani kwa wale wenye
kipato cha chini.
"Kikwazo kikubwa
kwa Tanzania ni ukosefu wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu, hali
hii inazuia Watu wenye Ulemavu kuendelea, kwa sababu bila ya vifaa
saidizi, Watu Wenye Ulemavu hawawezi kupata huduma muhimu za kijamii
kama elimu na mafunzo kwa ajili ya maisha ya kujitegemea na mchango wa
mchakato wa maendeleo wa taifa lao. Hii inajenga kikwazo kingine cha
ajira na bila kuwa na ajira yenye kipato, watu wenye ulemavu wataendelea
kubaki maskini," alisisitiza Dkt. Possi.
Mwisho, Dkt.
Possi alitoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuzisaidia nchi kama Tanzania
katika kupata vifaa saidizi vya watu wenye ulemavu, ikibidi kupata
teknolojia ya kuvitengeneza vifaa hivyo ndani ya nchi ili vipatikane kwa
urahisi.
0 comments:
Post a Comment