Home » » Ugonjwa wa Sumukavu wagundulika Dodoma.

Ugonjwa wa Sumukavu wagundulika Dodoma.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 




Na Ally Daud-Maelezo
Ugonjwa unaosababishwa na Sumukavu kwenye Mahindi ya chakula umegundilika katika Wilaya za Chemba na Kondoa Mkoani Dodoma baada ya kupeleka jopo la Wataalam waliofanya utafiti na kugundua kuwepo kwa ugonjwa huo.
 Akizungumza hayo katika mkutano wake na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi. Ummy Mwalimu amesema kwamba matokeo ya awali ya watafiti hao imeonyesha kwamba ugonjwa huo  umesababishwa na ulaji wa chakula kilichokuwa na sumukuvu na kuleta madhara.
“Hayo ni matokeo ya awali ya watafiti wa wizara yangu hivyo basi nasubiri matokeo ya vipimo vya damu na haja ndogo vilivyopelekwa kwa uchunguzi zaidi katika Maabara ya CDC, Atlanta iliyopo nchini Marekani na  matarajio yetu ni kupata majibu hayo katika kipindi kisichozidi wiki moja” aliongeza Bi Mwalimu.  
Aidha Bi. Mwalimu amesema kwamba  mpaka kufikia tarehe 24 Juni 2016, idadi ya wagonjwa imefikia 32, na idadi ya vifo imebakia 7. Hii ni baada ya kuongezeka kwa wagonjwa 11 katika kipindi cha wiki moja.
“Hadi jana kulikuwa na jumla ya wagonjwa 9 ambao wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Dodoma, na 14 wako katika Hospitali ya Wilaya ya Kondoa. Wagonjwa watatu waliolazwa Hospitali ya Mkoa Dodoma, na wawili waliolazwa Kondoa, bado hali zao ni tete” aliongeza Bi. Mwalimu.
Pamoja na hayo Bi. Mwalimu alisema kwamba  Serikali itaendelea kuimarisha mikakati ya kitaifa ya kupunguza uchafuzi wa sumukuvu katika vyakula, ikiwa ni pamoja na kujenga uwezo wa kupima vimelea hivyo katika damu na mkojo miongoni mwa taasisi za ndani ya nchi.
“ Tutaendelea kutoa matibabu kwa wananchi walioathirika na Ugonjwa huo, kwenye Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na Hospitali ya Wilaya ya Kondoa ili kudhibiti na kurudisha afya za wananchi katika kiwango kinachohitajikaaliongeza Bi. Mwalimu
Aidha Bi. Mwalimu  ametoa rai kwa wananchi na wakazi wa Dodoma  kwamba wanapaswa  kuchambua nafaka zilizoharibika (zilizooza, kuvunjika, zilizobadilika rangi), kukoboa mahindi kabla ya kusaga au kuacha kutumia nafaka zitakazoonekana kuharibika sana ili kuepukana na kiasi kilichozidi sumukavu kwenye nafaka.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa