SERIKALI imesema itawachukulia hatua za kinidhamu watumishi wa
halmashauri nchini waliohusika kusababisha watu wasio na sifa kulipwa
fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf).
Aidha, imesema itahakikisha viongozi waliochaguliwa kushiriki
utambuzi na ugawaji wa fedha hizo kwa kaya masikini, wakiwemo wa vijiji
waliohusika kuwaingiza kwenye orodha watu wasio na sifa kwa makusudi,
nao wanachukuliwa hatua zinazostahili. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais
(Tamisemi), George Simbachawene alisema hayo bungeni mjini hapa jana
alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Sabreena
Sungura (Chadema) aliyetaka kufahamu hatua zilizochukuliwa kwa
waliofanya makosa hayo.
“Kwa kuwa mpango huo umeleta malalamiko mengi na kumekuwa na
watumishi waliohusika kusababisha makosa hayo ya kuorodhesha wasio
masikini, je, Serikali inawachukulia hatua gani?” alihoji.
Akijibu, Simbachawene alisema, baada ya kutambua udanganyifu katika
kaya 25,446 kwamba hazikuwa na vigezo, Serikali imechukua hatua stahiki
ikiwa ni pamoja na kuagiza kuondolewa kwa watu hao kwenye orodha.
Alisema, kuhusu viongozi wa vijiji na wengine waliochaguliwa
kushiriki mpango huo wa kugawa fedha kwa kaya masikini, itaangaliwa
kuona endapo walifanya makusudi kuwaingiza watu wasio na sifa au
ilitokea bahati mbaya kwa sababu ya kutokuwa na takwimu sahihi, ili
hatua zichukuliwe.
Alisema kuwa makosa mengine yanaweza yakatokea lakini si kwa makusudi
ya aliyoyatenda, hivyo wanaangalia suala hilo pia kabla ya kuchukua
hatua zaidi. Katika swali lake la msingi, Sungura kupitia Mollel alitaka
kujua Serikali imejipangaje kutatua kero ya mgawanyo wa fedha hizo,
ambapo alieleza kuwa wananchi wengi wasio na uwezo wamekuwa hawazipati.
Simbachawene alisema, hasa katika Mkoa wa Kigoma, udanganyifu
umefanyika kwa kiasi kikubwa na wahusika wote watachukuliwa hatua
zinazostahili za kisheria, kuhakikisha suala hilo haliendelei kutokea.
Alieleza kuwa utambuzi wa kaya za walengwa wa mpango huo ulianza
Novemba, 2013 na hadi sasa umekwishaandikisha kaya milioni moja na laki
moja katika halmashauri 159 za Tanzania Bara, pamoja na wilaya zote za
Unguja na Pemba.
Kwa mujibu wa Simbachawene, kaya hizo zinapata ruzuku kwa utaratibu
wa uhawilishaji fedha baada ya kutimiza masharti ya kupeleka watoto
shule na kliniki. Alisema, wakati mpango wa kunusuru kaya masikini
unaanza ulipanga kufikia asilimia 70 ya vijiji, mitaa na shehia za
halmashauri ambavyo vimefikiwa zilijaziwa dodoso ili kukusanya taarifa
zaidi za kaya na hatimaye ziliandikishwa kwenye daftari la walengwa na
kuanza kupokea ruzuku.
Alisema, maeneo yote 161 ya utekelezaji ambayo ni halmashauri 159 za
Tanzania Bara, Unguja na Pemba, zimeshaondoa kaya zisizostahili kuwa
kwenye orodha ya walengwa. “Jumla ya kaya 25,446 zimekwishaondolewa
kwenye mpango huo kwa sababu mbalimbali zikiwemo vifo, kukosa vigezo vya
kuwa kaya masikini na kuondolewa kwa wajumbe wa kamati za mpango na
viongozi wa vijiji, mitaa na shehia katika orodha ya kaya
masikini,”alisema.
Chanzo Gazeti La Habari Leo
0 comments:
Post a Comment