Home » »
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Tetemeko kubwa laikumba Dodoma

Sehemu ya eneo la Itiso
WAKAZI wa Dodoma jana asubuhi waliingiwa na taharuki baada ya mji huo kukumbwa na tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa kipimo cha Richter 5.1.
Akizungumza jana ofisini kwake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Jiolojia Tanzania, Profesa Abdulkarim Mruma alisema tetemeko hilo lililotokea saa 12.01:15 asubuhi wakati wananchi wengi wakiwa wamelala na ni kubwa ukilinganisha na matetemeko ambayo yamezoeleka kutokea yenye ukubwa wa Richter 3.
Profesa Mruma alisema kitovu cha tetemeko hilo kilikuwa katika Bonde la Haneti - Itiso wilayani Chemba mkoani Dodoma.
Pia alisema kutokana na ukubwa wa tetemeko hilo, mikoa mingine ambayo ipo karibu na eneo la chanzo cha tetemeko nayo imeathirika na kuitaja mikoa hiyo iliyoathirika kuwa ni pamoja na Tanga, Dodoma, Singida upande wa mashariki na Manyara.
Alisema tetemeko hutokea katika miamba migumu yenye madini ya dhahabu. Akielezea chanzo cha tetemeko, Profesa Mruma alisema limesababishwa na kupasuka kwa matabaka ya ardhi, na hutokea kutokana na kuteleza kwa mapande hayo ambapo husababisha mtikisiko.
Alisema mapande ya ardhi ya Itiso ambayo yapo katika mtawanyiko wa Bonde la Ufa la Arusha yanaendeleza kuteleza na kwamba tetemeko hilo ni endelevu kwani bonde hilo la Itiso linazidi kusogea.
Alishauri watu wanaojenga maghorofa katika mkoa wa Dodoma kuzingatia ushauri wa Wakala wa Jiolojia, kwani athari za kujenga majengo marefu kwa mkoa huo bado zipo pale pale.
Aliwataka wanaojenga ghorofa waombe ushauri kwao kwani ukitaka kujenga ghorofa zaidi ya mbili ni lazima jengo liwe pana.
Kwa upande wa Mjiolojia Mwandamizi kutoka Wakala wa Jiolojia Tanzania ambaye pia ni mtaalamu wa matetemeko, Gabriel Mbogoni alisema tetemeko hilo limetokea maeneo ya Haneti kilometa 11 mashariki mwa mji wa Haneti Wilaya ya Chemba ambao upo kilometa 79 kutoka kaskazini mashariki mwa mji wa Dodoma.
“Hatujapata taarifa zozote za madhara labda kwa sababu bado ni mapema,” alisema Mbogoni.
Chanzo Na Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa