Na Beatrice Lyimo-MAELEZO
06/09/2016
Serikali ya Tanzania haiwezi na haina nia ya kufuta michezo nchini kwa sababu yeyote ile.
Kauli
hiyo imetolewa leo mjini Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa
na Michezo Mhe. Nape Nnauye alipokuwa akijibu swali la Mhe. Venance
Mwamoto ambaye alihoji kutaka kujua kwa nini Serikali isifute Michezo
nchini.
Akijibu
swali hilo Mhe. Nape alisema kuwa nia ya Serikali ni kuendeleza Sekta
ya Michezo kwa maendeleo ya Taifa kwa kuwekeza katika miundombinu ya
michezo, Elimu ya Michezo na kushirikiana na wadau wengine na
kuhakukisha sekta ya michezo inaendelezwa.
“Naamini
kuwa swali lake limelenga kupata maelezo ya kwanini michezo haiendelei
kwa kasi wanayotamani wanamichezo wengi hapa Tanzania na wala siamini
kuwa anayo nia ya kutaka Serikali ifute michezo kwa kuwa anafahamu fika
umuhimu wa michezo kwa Taifa pamoja na wananchi kwa ujumla”, Alisema
Mhe. Nape.
Waziri
Nape aliongeza kuwa Serikali kupitia Wizara yake itaendelea kutenga
fedha kupitia Bajeti ya Wizara na vyanzo vingine kadri iwezekanavyo ili
kuendeleza michezo katika ngazi mbalimbali.
Aidha,
alitoa wito kwa wadau wa michezo, ikiwemo Serikali za Mitaa, Wizara ya
Elimu Sayansi na Teknolojia, waheshimiwa wabunge, Sekta binafsi na wadau
wengine kuibua vipaji vya michezo kwa watoto kuanzia umri mdogo na
kuviendeleza.
Akizungumza
kuhusu mpango wa Serikali kudhibiti mavazi yasio na staha kwa baadhi ya
wasanii nchini, Waziri Nape amesema kuwa Wizara kupitia Baraza la Sanaa
la Taifa imekuwa ikitoa elimu kwa wasanii mara kwa mara juu ya umuhimu
wa maadili katika sanaa na namna ya kubuni kazi za sanaa zenye ubora
unaozingatia maadili ya nchi na jamii.
Pia
Waziri Nape ametoa wito kwa wananchi kuhakikisha wasanii nchini
wanazingatia nidhamu katika mavazi wanayoyatumia katika kazi zao za
sanaa na kuwataka Watanzania kutunza na kulinda maadili na utamaduni wa
Mtanzania.
“Ikiwa
jamii inayakataa mavazi hayo ili kulinda maadili itapelekea wasanii hao
kuona mavazi hayo hayatakiwi, endapo jamii itaonyesha kuyakuwali mavazi
hao itapelekea wasanii hao kuona ni kitu cha kawaida na kuzidi
kutozingatia maadili,” alifafanua Waziri Nape.
Mavazi
ni moja ya utambulisho unaozingatiwa katika Sera ya Taifa ya Utamaduni
ya mwaka 1997 inayomtaka Mtanzania ana wajibu wa kulinda mila na desturi
sambamba na kuhakikisha maadili yanalindwa na wanawake hawadhalilishwi
kupitia kazi za sanaa.
0 comments:
Post a Comment