Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma.
Wabunge
wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamepewa semina kuhusu
Mkataba wa Makubaliano ya Ushirikiano wa Kiuchumi kati ya Jumuiya ya
Afrika Mashariki na Jumuiya ya Ulaya (EPA) ili wapate uelewa na hatimaye
kuishauri Serikali juu ya suala hilo.
Semina
hiyo imetolewa kwa Wabunge leo mjini Dodoma na wataalamu kutoka Chuo
Kikuu cha Dar es Saalam akiwemo Prof. Palamagamba Kabudi, Dkt. Ng’waza
Kamata na Dkt. John Jingu pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda,
Biashara na Uwekezaji, Prof. Adolf Mkenda.
Akifungua
semina hiyo, Spika Mhe. Job Ndugai amesema kuwa anatambua umuhimu wa
mkataba huo ni vema Wabunge watumie fursa ya semina hiyo ili
watakapofika kwenye mjadala wenyewe ndani ya Bunge wawe na uelewa mpana
kwa manufaa ya nchi.
“Natambua
kwamba majadiliano haya yamefanyika sana hasa katika vikao vya Bunge
lililopita, lakini kwa kuwa wabunge wengi ni wapya tumeona kuna umuhimu
wa kuandaa Semina hii ili tuweze kupata elimu na kuongeza uelewa wa
jambo hili kabla ya kuujadili rasmi ndani ya Bunge letu”, alisema
Ndugai.
Ameongeza
kuwa semina hii pia itawapa wabunge nafasi ya kuuliza maswali na
kufanya majadiliano ya jumla ili kupata ufafanuzi wa kina juu ya mambo
mbalimbali yanayohusu mkataba huo, hiyo yote ikiwa ni njia ya
kuwaelimisha ili siku ya majadiliano rasmi watoe mapendekezo
yatakayoleta tija na manufaa kwa nchi yetu.
Kwa
upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji,
Prof. Adolf Mkenda alipokuwa akiwasilisha mada juu ya chimbuko,
mustakabali na uchambuzi wa EPA amesema hiyo ni namna bora ya
kuwashirikisha na kuwapa uelewa Wabunge ili waweze kujadili mkataba huo
kwa manufaa ya taifa.
Nao
wataalam kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wamewashauri wabunge
kutumia semina hiyo kama muongozo utakaowawezesha kuboresha mjadala wao
wakati wa kutoa michango yao ndani ya Bunge ili waweze kutoa majibu
sahihi siku ya kuujadili mkataba huo.
Mswada
huo unatarajiwa kuwasililishwa Bungeni Novemba 10 mwaka huu ambapo
mjadala huo utapelekea kuishauri Serikali kuhusu hatma ya mkataba huo.
0 comments:
Post a Comment