Na Dotto Kwilasa, JamhuriMedia, Dodoma

BAADA ya kimya cha muda mrefu kuhusu nani anachukua nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Taifa (CCM) jibu limepatikana ambapo anatarajiwa kupatikana kati ya January 18 au 19 mwaka huu.

Hatua hii ni mara baada ya aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Abdulrahman Kinaana kutangaza kustaafu kwenye nafasi hiyo tangu Julai mwaka jana kwa madai ya kutaka kupumzika ambapo Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan aliliridhia ombi lake.

Akizungumza leo Januari 7,2025 Jijini Dodoma, Katibu wa NEC,Itikadi , Uenezi na Mafunzo wa Chama hicho Amos Makala ameeleza kuwa nafasi ya Makamu Mwenyekiti huwa haigombewi wala kujazwa fomu bali hutokana na mapendekezo ya Mkutano Mkuu na halmashauri kuu ya CCM.

“Niwaombe wanachama watu kuachana na taharuki zinazoendelea kwenye mitandao ya kijamii kuhusu mrithi wa Makumu Mwenyekiti wa chama Abdulahman Kinana, nafasi hii haigombewi ila inapendekezwa, ” ameeleza Makala.

Makala amewaambia waandishi wa habari kuwa kwa sasa hakuna mchakato wowote wa mrithi wa nafasi hiyo ambaye atapatikana baada ya mapendekezo ya jina katika kikao cha Kamati kuu na Halmashauri kuu Taifa.