Home » » Kuomba fedha LAPF: Wabunge waumbuana

Kuomba fedha LAPF: Wabunge waumbuana

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mbunge Freeman Mbowe  

Bunge jana liligeuka uwanja wa kurushiana makombora pale wabunge walipoumbuana kuhusu baadhi yao kudaiwa kuwa ombaomba katika Mfuko wa Pensheni kwa Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (LAPF).
Kuumbuana huko kuliegemea taarifa ya Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu kuwalipua baadhi ya mawaziri na wabunge kwa kuchota fedha katika mfuko huo.
Sakata hilo lilienda mbali zaidi baada ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe kulipuliwa kuwa anadaiwa zaidi ya Sh1 bilioni na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na tayari kuna hati ya kumkamata.
Hata hivyo, Mbowe alipoulizwa jana ofisini kwake bungeni alisema: “...Sina taarifa yoyote ya kukamatwa. Nipo hapa bungeni mbona sijakamatwa? Muulizeni aliyesema awaeleze imetolewa lini na nani,” alisema Mbowe.
Wabunge hao walianza kuumbuana baada ya Mbunge wa Mbinga Magharibi (CCM), John Komba kutaka mwongozo wa Spika, akidai Lissu alimtaja kuwa naye ni miongoni mwa wabunge waliochota fedha LAPF.
“Kati ya wabunge hao wanaofilisi mashirika ya umma, mimi sikumbuki wala sijui LAPF iko wapi wala ofisini kwa mkurugenzi wake wala kwa mfanyakazi wake na sijachukua fedha yoyote LAPF,” alisema.
Akionyesha kukerwa, Komba alisema anachokumbuka Mfuko wa Maendeleo wa Nyanza ambao ni wadau wa LAPF waliomba msaada wa kununua boti na walipewa Sh1.5 milioni... “Leo Lissu amekuja hapa anawadanganya watu kuwa mimi nimehusika kutoa mapesa LAPF, sijui huu ni wendawazimu ama nini?... Hizi ni siasa za majitaka kabisa naomba mwongozo wako.”
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alijibu hoja hiyo akisema wabunge kuomba katika mashirika hayo si jambo la ajabu na kwamba yeye mwenyewe aliomba kwa barua.
“Nilitaka kusema jambo hili si kubwa kiasi hiki kwa sababu fedha hizi zipo kwa ajili ya maendeleo...”
Hata hivyo, Lissu alipopewa fursa ya kujibu alipigilia msumari akisema wabunge ndio wenye jukumu la kusimamia mifuko hiyo na kwamba kama wanachukua fedha za mifuko hiyo wanaingia moja kwa moja katika mgongano wa kimasilahi.
Aidha, alisema LAPF kwenye fungu hilo la msaada kwa jamii inatoa kwa wabunge wa CCM pekee yake... “Kwa sababu wabunge waliopewa fedha na nyaraka zake zipo ni hao wanaopiga kelele kina Pindi Chana, Mwigulu Nchemba, wanaochukua fedha ni wa CCM tu.”
Alihoji kutumika kwa fedha za LAPF kununua jezi katika Jimbo la Chato linaloongozwa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli.
Pia alihoji Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ambayo hutengewa bajeti kununuliwa printa na kompyuta na LAPF.
Katika ufafanuzi wake, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alisema hakuna mtu anayepewa kitu bila kuomba.
“Kwenda kuomba misaada si tu katika mifuko ya jamii tu, bali hata katika maeneo mengine kwa ajili ya maendeleo ya majimbo yao inaruhusiwa. Katika mifuko ya jamii kuna sera ambazo zimepanga kusaidia katika elimu, afya na masuala mengine ya kiuchumi katika jamii.”
Kabaka alisema kama Lissu hajaomba msaada wa fedha hizo, asilazimishe kwamba mifuko hiyo inasaidia wabunge wa eneo moja.
“Si vizuri kusema kwa sababu ni masuala binafsi lakini kuna waliokopa pesa kwenye mifuko ya jamii ukiwamo mfuko wa NSSF ambao uko chini ya wizara yangu,” alisema Kabaka.
Alisema kuwa kuna hati ya kumkamata kumchukua mbunge aliyekopa bila kurejesha na kwamba hizo ndizo fedha ambazo si halali.
Wakati Kabaka akisema si vizuri kumtaja mbunge, kelele za wabunge zilisikika zikimtaja Mbowe na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi, Hawa Ghasia, alimtaja Mbowe kuwa ndiye anayedaiwa deni... “Mheshimiwa Kabaka hakumtaja lakini anayedaiwa ni Mbowe aende akalipe deni hilo.”
Baadaye, Nchemba aliomba mwongozo wa Spika na kueleza kuwa kanuni za Bunge zinamkataza mbunge kuzungumzia jambo ambalo ana masilahi binafsi... “Mheshimiwa Lissu ni wakili lakini anamtetea mfanyakazi aliyefukuzwa na LAPF kwa matumizi mabaya ya madaraka, leo anaongea vibaya kuhusu shirika hilo, nadhani kuwa anakiuka.”
Alisema kanuni hiyo inamtaka aweke wazi kwanza masilahi yake katika mfuko huo kabla ya kuanza kuzungumza.
“Leo hii tunavyoongea baada ya Katibu Mkuu wa CCM kupita jimboni kwangu na kukuta kijiji kimoja tu kina umeme nadhamiria kuandika mradi mwingine niombe solar (umeme wa jua) nipeleke,” alisema.
Alisema kuwa ataomba fedha hizo kupitia mashirika hayo ya kijamii na kwamba ni kazi ya mbunge kuhakikisha kuwa fedha zinazotengwa kwa ajili ya kuisaidia jamii zinatumika ipasavyo.
Alitaka Bunge lichukue hatua kwa mbunge (Mbowe), ambaye Kabaka alisema ana hati ya kukamatwa kwa kutokulipa zaidi ya Sh1 bilioni.
Hata hivyo, Ndugai alisema atatoa ufafanuzi kuhusu mwongozo huo baadaye.
Juzi, Mkurugenzi Mkuu wa LAPF, Eliud Sanga alisema mfuko huo hulazimika kuwapa msaada zaidi wabunge wa CCM kwa kuogopa kuwa wakiegemea kwa wa upinzani wataonekana wanawapigia debe.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa