Home » » NAPE ALAANIWE KWA KUTUITA BOKO HARAM'

NAPE ALAANIWE KWA KUTUITA BOKO HARAM'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Mbunge wa viti maalumu kwa tiketi ya CUF, Amina Abdallah Amour amemjia juu katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Nape Nnauye kwa kuufananisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na kundi la Boko Haramu na kutaka alaaniwe.
Ukawa iliundwa wakati wa Bunge Maalumu la Katiba na unahusisha wajumbe kutoka vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na CUF.
Akizungumza bungeni mjini Dodoma juzi, mbunge huyo alisema kauli ya Nnauye ni ya uchochezi na inapaswa kulaaniwa.
Mbunge huyo alikuwa akichangia hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Wanawake, Jinsia na Watoto kwa mwaka 2014/2015 iliyowasilishwa na waziri wake, Sophia Simba.
“Gazeti la Uhuru (jana) lilimnukuu Nape Nnauye akisema Ukawa ni sawa na Boko Haramu… Hii ni kauli chafu na ya uchochezi. Haikubaliki na ninailaani kwa nguvu zangu zote,” alisema.
Mbunge huyo alihoji “wazazi wao hawajui watoto wao wanaishije, wanakula nini wala wanalala vipi…. Leo hii Nape Nnauye amethubutu kusema Ukawa ni sawa na Boko Haramu?”
Hata hivyo, wakati akihoji hivyo, baadhi ya Wabunge wa CCM nao walisikika wakihoji “na Intarahamwe Je?”.
Ukawa ilitumia jina hilo la Interahamwe wakati mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akitangaza uamuzi wa kundi hilo kujitoa kwenye Bunge la Katiba, akiifananisha CCM na kundi hilo la nchini Rwanda.
Katika gazeti hilo, Nnauye amenukuliwa akisema Ukawa ni kundi hatari linaloeneza chuki na kusambaza uongo kwa Wananchi kwa nia ya kuwagawa na kusema silaha wanazotumia ni zaidi ya Boko Haramu.
Nnauye anadaiwa kutoa kauli hiyo katika mkutano wa hadhara uliofanyika mkoani Tabora, akisema silaha za uongo wanazotumia viongozi wa Ukawa ni hatari zaidi kuliko silaha za moto zinazotumiwa na Boko Haramu.
Viongozi wa CCM na wale wa Ukawa wamekuwa wakizunguka nchi nzima kufanya mikutano ya hadhara kufafanua kile kilichojitokeza ndani ya Bunge la Katiba na kusababisha Ukawa kususia Bunge hilo.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa