Home » » WAFUATA HUDUMA ZA AFYA KILOMITA TISA

WAFUATA HUDUMA ZA AFYA KILOMITA TISA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
WANANCHI wa Kijiji cha Chonde, Kata ya Makanda, Tarafa ya Mundemu, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma, wanalazimika kufuata huduma za afya umbali wa kilomita tisa, kutokana na kijiji chao kutokuwa nazo tangu uhuru.
Kijiji hicho kina kaya 684 zenye idadi ya watu 3,426 ambapo kati yao wanaume ni 1,606 na wanawake 1,820.
Kutokana na kadhia hiyo, wajawazito hulazimika kujifungulia njiani hali inayochangia watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano kukosa huduma bora za kiafya kama inavyostahili.
Taarifa hiyo ya kusikitisha ilitolewa na Katibu wa CCM Kata ya Mundemu, Daud Mrutu wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa zahanati katika kijiji hicho, iliyoandaliwa na Diwani wa Kata ya Makanda, Anton Lyamnda (CCM).
Mrutu alisema kuwa kutokana na kuwepo kwa adha kubwa ya wanakijiji kutembea kilometa tisa kutafuta huduma ya afya, wakazi wa kijiji hicho wamekuwa wakikosa haki yao ya kupatiwa huduma ya matibabu kwa ufasaha.
Alisema kuwa kutokana na Halmashauri ya Bahi kuonekana kuwatelekeza wanakijiji hao, kwa sasa hawana imani tena na halmashauri yao.
“Katika mwaka wa fedha 2011/12 wilaya ilituma barua kwenye Kijiji cha Chonde kuwa imekitengea bajeti ya sh. milioni 65 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati, lakini hakuna utekelezaji wa aina yoyote ulioonekana.
“Pia katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2013/14, wilaya ilitenga bajeti ya sh. milioni 30 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati, lakini hadi leo hatujaona utekelezaji wowote. Wananchi wamekosa imani na halmashauri yao,” alisema Mrutu.
Diwani Lyamnda alisema ili jengo la zahanati liweze kukamilika litagharimu sh. milioni 98 ambapo hadi sasa zimetumika sh. milioni 7.8.
Katika harambehe hiyo ambayo ilihudhuriwa na Mbunge wa Bahi, Omar Badwel (CCM), mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa, Ally Nyange, madiwani pamoja na wananchi, zilichangwa sh. miloni 11.1 ambapo kati ya hizo sh. milioni 9.8 zilikuwa ahadi.
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa