Spika wa Bunge, Anne Makinda.
Hata hivyo, licha ya Spika kuwakana kuwa siyo wenyeviti halali wa
kamati hizo, baadhi yao ‘wamemtunishia misuli’, baada ya kuamua
kuendelea kuongoza vikao vya kamati zao.
Tafsiri hiyo imetokana na kauli ya Spika Anne Makinda, aliyoitoa kwa waandishi wa habari jana kwamba ‘anatambua wameshajiuzulu.’
Aidha, wakati msimamo wa Spika Makinda ukiwa hivyo, jana waandishi
wa habari walishuhudia wenyeviti hao wakiendelea kuongoza vikao vya
kamati zao.
Wenyeviti waliotakiwa kujiuzulu ni Andrew Chenge (Bajeti), William
Ngeleja (Katiba, Sheria na Utawala) na Victor Mwambalaswa (Nishati na
Madini). Hata hivyo, taarifa zinaeleza kuwa Chenge amekwishaachia
wadhifa huo.
Ngeleja alitakiwa ajiuzulu kwa kuwa alipata mgawo wa Sh. milioni
40.2 zinazodaiwa kuchotwa katika akaunti ya Tegeta Escrow huku Chenge
akigawiwa Sh. bilioni 1.6. Aidha, Mwambalaswa alitakiwa ajiuzulu kwa
kuwa kamati yake inasimamia sekta ya Nishati na Madini yaani Wizara ya
Nishati na Madini pamoja na mashirika yake.
Akijibu maswali ya waandishi wa habari katika ofisi ndogo za Bunge
jijini Dar es Salaam jana, Spika Makinda alisema azimio namba 8 la Bunge
liliwataka wenyeviti hao wajiuzulu wenyewe na kwamba anaamini
wamekwishafanya hivyo.
"Ukiniuliza mimi nitakuambia watu wote walishajiuzulu, mimi najua
wamejiuzulu. Azimio lilitaka wajiuzulu siyo wawajibishwe," alisema.
Alipoulizwa ikiwa wameandika barua ama la alisema: "Barua ya nini
wakati walitakiwa wajiuzulu na wajumbe wa kamati wachague Mwenyekiti
mwingine? Ukiniuliza habari ya barua mimi sijui."
Makinda pia alisema kuwa yeye ndiyo mtu wa mwisho kutoa maamuzi na
jambo la kuwa baadhi ya wenyeviti kuongoza vikao vya kamati halitambui.
"Habari za hao kuongoza vikao sijui ila mimi ndiyo nasema kuwa
tayari wameshajiuzulu kutokana na jinsi azimio la Bunge linavyosema,"
alisema Makinda.
MAAZIMIO YA BUNGE
Maazimio kadhaa yalitolewa yakiwamo ya kuwawajibisha kwa kutengua
uteuzi wa Profesa Muhongo, Maswi, Profesa Tibaijuka na Jaji Werema
ambaye amejiuzulu mwenyewe.
Wengine waliopendekezwa kuvuliwa uongozi wao kwenye kamati za Bunge
ni Endrew Chenge (Bajeti), William Ngeleja (Katiba, Sheria na Utawala)
na Victor Mwambalaswa (Nishati na Madini). Chenge akipewa Sh. bilioni
1.6 na Ngeleja Sh. milioni 40.2, kwa mujibu wa taarifa ya CAG na Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu (PAC).
Pia Bunge liliazimia, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(Takukuru), Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na
usalama, vichukue hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi kwa watu
wote waliotajwa kuhusika na vitendo vyote vya jinai, kuhusu miamala ya
akaunti ya Tegeta Escrow, na watu wengine watakaogundulika baada ya
uchunguzi mbalimbali unaondelea katika vitendo hivyo vya jinai.
Miongoni mwao ni mmiliki wa kampuni ya PAP, Harbinder Singh Sethi,
James Rugemalira wa VIP Engineering Ltd, Jaji Werema, Profesa Muhongo,
Maswi, wajumbe wa Bodi ya Tanesco, ambao inasemwa kuwa walihusika kwa
namna moja au nyingine kufanikisha kufanyika kwa miamala haramu ya fedha
katika akaunti ya Tegeta Escrow kwenda PAP na VIP Engineering and
Marketing Ltd.
Kuhusu ushiriki wa majaji katika kashfa hiyo, ni kwamba Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, imeweka utaratibu
mahususi wa Tume ya Kijaji ya Uchunguzi kuchunguza tuhuma za utovu wa
nidhamu wa maadili dhidi ya Jaji Aloysius Mujulizi na Jaji Profesa Eudes
Ruhangisa wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Bunge liliazimia kushughulikia nidhamu ya majaji ambao kwa mujibu
wa Katiba hiyo, unamtaka Rais aunde Tume ya Uchunguzi ya Kijaji
kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya majaji.
Pia Bunge liliazimia serikali iandae na kuwasilisha Muswada wa
Marekebisho ya Sheria iliyounda Takukuru kwa lengo la kuanzisha taasisi
mahsusi itakayoshughulikia, kupambana na kudhibiti vitendo vya rushwa
kubwa, ufisadi, na hujuma za uchumi zinazotishia uhai wa Taifa kiuchumi,
kijamii na kisiasa kutokana na kushamiri kwa vitendo hivyo.
Kadhalika Serikali iangalie uwezekano wa kununua mitambo ya kufua
umeme ya IPTL na kuimilikisha kwa Tanesco kwa lengo la kuokoa fedha za
shirika hilo.
Bunge lilishauri kuwa hatua za haraka zichukuliwe na Kamati husika za Bunge kabla ya kuanza kwa mkutano wa 18 wa Bunge.
Novemba mwaka jana wakati wa kikao cha 16 na 17, Bunge liliazimia
kwamba katika sakata la akaunti ya Tegeta Escrow wahusika wote
wawajibishwe.
WALIOFIKISHWA KORTINI
Hadi sasa watumishi watano wa serikali wamefikishwa kizimbani kwa tuhuma za kupokea mgawo wa fedha za Escrow.
Vigogo wa kwanza kufikishwa mahakamani ni Teophil John, Mhandisi
Mwandamizi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Mkurugenzi wa
Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa
Teophil walifikishwa mahakamani kwa madai ya kupokea rushwa kutoka kwa
James Rugemalira.
Wengine ni Mkurugenzi wa Fedha wa Benki Kuu (BoT), Julius Angello;
Mwanasheria Mwandamizi wa Tanesco, Steven Urassa na Meneja wa Misamaha
ya Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kyabukoba Mutabingwa.
CHINA YALISAIDIA BUNGE
Wakati huo huo, Spika wa Bunge, Anne Makinda, amesema mhimili huo
utaanza kutumia Teknolojia ya Mawasiliano (Tehama) kuendesha shughuli
zake na kwamba lengo ni kuwawezesha wabunge kutumia mtandao wawapo
bungeni.
Spika Makinda alitangaza mageuzi hayo jana jijini Dar es Salaam,
alipokuwa akipokea msaada wa vifaa vya Tehema kutoka kwa Balozi wa China
nchini, Lu Youqing.
Alisema mkakati huo ukifanikiwa, utaongeza ufanisi kwa kuwa kila
mbunge atakuwa na kompyuta ndogo (laptop) ambayo itakuwa na taarifa za
shughuli zote za siku husika kwa wakati.
Aliishukuru serikali ya China kwa msaada huo na kuahidi kwamba
Bunge la Tanzania limeazimia kuimarisha uhusiano na Bunge la nchi hiyo.
Kwa upande wake, Balozi Youqing, alisema vifaa hivyo ni mashine
kubwa za kudurufu (10), mashine za kuchapa (10), fax (10), scanner
(10), kamera (10), kompyuta mpakato (23), Ipad (13) na vifaa vingine
muhimu.
Alisema urafiki wa Tanzania na China ni wa historia hivyo miongoni mwa majukumu yake ni kuhakikisha unaendelea kudumu.
CHANZO:
NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment