Home » » Serikali kutobinafsisha shirika la Tafico

Serikali kutobinafsisha shirika la Tafico

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Walemavu, Antony Mavunde.
SHIRIKA la Uvuvi Tanzania (Tafico) limeondolewa katika mchakato wa kubinafsishwa na sasa Serikali iko katika mpango wa kulifufua. Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Ajira, Kazi na Vijana, Anthony Mavunde alisema hayo jana alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile (CCM).
Katika swali hilo lililoulizwa kwa niaba yake na Mbunge wa Viti Maalumu, Mariam Kisangi (CCM), Dk Ndugulile alitaka kujua Serikali ina mpango gani wa kufufua shirika hilo ambalo zamani lilikuwa na makao makuu yake Kigamboni, Dar es Salaam.
Pia alitaka kuelezwa Serikali imejipanga vipi kusimamia uvuvi katika bahari kuu ili Taifa linufaike na mapato. Akifafanua majibu hayo kwa kuelezea historia ya shirika hilo, Mavunde alisema Tafico ilianzishwa mwaka 1974 na kukabidhiwa kwa lengo la kuendesha shughuli za uvuvi kibiashara.
Kwa mujibu wa Mavunde, mwaka 1996 shirika hilo liliwekwa chini ya iliyokuwa Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC) kwa ajili ya utaratibu wa ubinafsishaji. Mwaka 2007 kwa mujibu wa Mavunde, shirika hilo liliondolewa kwenye orodha ya mashirika yaliyotakiwa kubinafsishwa PSRC na kurejeshwa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa ajili ya kuendeleza ubinafsishaji wake.
Hata hivyo, mwaka 2007, Mavunde alisema Baraza la Mawaziri lilisitisha uuzwaji wa shirika hilo na kuelekeza kuwa mali zake zisizohamishika ikiwemo ardhi zibaki kwa ajili ya matumizi ya serikali.
Kwa sasa Mavunde alisema wizara kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya uvuvi, inaendelea na mpango wa kufufua shirika hilo ikiwa ni pamoja na kuwasilisha mapendekezo katika Baraza la Mawaziri kwa hatua husika.
Chanzo Gazeti La Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa