Home » » Wananchi wasalimu amri kwa mwekezaji, wakubali kumpisha achimbe madini ya shaba

Wananchi wasalimu amri kwa mwekezaji, wakubali kumpisha achimbe madini ya shaba



Dodoma
Zaidi ya wananchi 29 wa Kijiji cha Kinusi Wilaya ya Mpwapwa waliokuwa na mashamba na makaburi katika Mlima Kitononge wamekubali kumpisha mwekezaji aliyegundua madini ya Shaba baada ya kuwapo kwa mvutano wa fidia za kuhamishwa katika eneo hilo.
Mwekezaji huyo ambaye ni Kampuni ya C.S.N Company amekubali kuchangia shughuli mbalimbali za maendeleo katika kijiji hicho, jambo ambalo wananchi hao wamekubaliana naye kuanza kuchimba madini hayo.
Mwenyekiti wa kijiji hicho, Ussa Mnyama alisema tayari wananchi 29 wameshalipwa fidia ya mashamba na makaburi katika mlima huo ili kumpisha mwekezaji huyo ambaye amesema wamekubaliana kukisaidia kijiji hicho katika shughuli za kimaendeleo.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Juma Chibaya alikiri kumalizana na wananchi hao ambapo zaidi ya Sh40 milioni zilitumika kuwalipa ili kuwapisha wao kuchimba madini katika mlima huo.
Chibaya alisema pamoja na mambo mengine lakini wamekubaliana na uongozi wa kijiji hicho kusaidia shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo kwa kuanzia wataanza na kutengeneza madawati 100 ya Shule ya Msingi Kinusi.
Alisema wananchi hao wamepongeza hatua ya mwekezaji kufikia hatua ya makubaliano na wao na pia kitendo cha kukubali kusaidia shughuli mbalimbali za kijamii kwa ajili ya maendeleo ambayo ni muhimu katika jamii kwani ni jambo la muhimu zaidi kwao. (Masoud Masasi).
Chanzo: Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa