Home » » Serikali: Wapo wanaume siyo rijali

Serikali: Wapo wanaume siyo rijali

Dodoma. Serikali imekiri kuwapo wanaume ambao mbegu zao hazina uwezo wa kuwapa mimba wanawake na kwamba, imekuwa ikiendelea kutoa elimu mara kwa mara.
Hayo yalisemwa jana na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid alipojibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Kidawa Saleh (CCM).
Mbunge huyo alitaka kujua iwapo Serikali haioni umuhimu wa kutoa elimu kwa wanaume ili wajue wapo ambao mbegu zao hazina uwezo wa kumpa mwanamke mimba na kwamba, tatizo hilo siyo kwa wanawake pekee.
“Kwa kuwa wanawake wengi wamekuwa wakiiba watoto kutokana na kunyanyaswa na waume zao kwa kutokuwapatia watoto, je Serikali kwa nini isitoe elimu kwa wanaume?” alihoji mbunge huyo.
Dk Seif alikanusha kuwa siyo wanawake pekee wenye matatizo ya kushindwa kushika mimba, bali zipo sababu kwa pande zote mbili za kushindwa kutunga mimba.
Alisema wamekuwa wakitoa elimu ya uzazi mara kwa mara vituo vya tiba na kupitia vyombo vya habari, kuhusu jambo hilo.
Awali, katika swali la msingi, Kidawa alitaka kujua sababu za kuongezeka kwa tatizo hilo miaka ya karibuni.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Pereira Ame Silima alisema kuanzia Januari, 2011 hadi Septemba mwaka huu kulikuwa na matukio 310 ya wizi wa watoto nchi nzima, kati yao wa kike ni 128 na wa kiume 182.
Alisema watoto 177 kati ya 310 walioibwa, walipatikana baadhi yao wakiwa hai.
na wengine wakiwa watuhumiwa 174 wakiwemo wanaume 101 na wanawake 73 walikamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa