Home » » Kufeli mitihani si mwisho wa safari, jipange

Kufeli mitihani si mwisho wa safari, jipange

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Februari mwaka huu, Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), lilitangaza matokeo ya mtihani wa kidato cha nne wa mwaka 2013.
Katika matokeo hayo, wanafunzi 151,187 walipata daraja sifuri, sawa na asilimia 42.91 ya watahiniwa 404,083 waliofanya mtihani huo.
Bila shaka idadi ya watahiniwa waliofeli ni kubwa na huenda wapo baadhi yao waliokata tamaa ya kuendelea na masomo baada ya kufeli kwa kiwango hicho kikubwa.
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mpwapwa iliyopo Dodoma, Rukonge Mwelo anasema umefika wakati kwa Serikali kuanzisha masomo ya ujasiriamali kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili wale wanaofeli wasibaki njiapanda.
“Kuna wanafunzi wamepata sifuri kwenye mitihani yao lakini hao hao wakija kwenye kazi za mikono wanapata alama A,” anasema.
Anasema baadhi ya wanafunzi wanashindwa kufanya vizuri katika mitihani kutokana na kuwepo kwa mazingira mabaya ya kujifunzia, ikiwamo kukosekana kwa walimu na vifaa vya kujifunzia.
Mwelo anaongeza kusema: “Kama kila wilaya itakuwa na kituo cha mafunzo ya ufundi stadi kwa watu waliofeli itasaidia sana, kwa sababu kufanikiwa siyo lazima ufike kidato cha nne.”
Anatoa mfano wa wanafunzi walioacha shule na kujiingiza katika biashara ya kusafirisha abiria kwa kutumia pikipiki baada ya kukatishwa tamaa na wenzao waliopata sifuri.
Hata hivyo, mzazi Marry Kashinde anasema hata ujasiriamali nao unahitaji elimu ili mtu aweze kufanikiwa.
Anasema baada ya binti yake kufeli aliomba afunguliwe biashara ya kuuza nguo za watoto, lakini alishindwa kuendea kwa kukosa ujuzi wa kazi hiyo.
“Mimi nina ushahidi wa kutosha kuwa hata ujasiriamali unahitaji elimu, siyo lazima iwe elimu rasmi lakini mtu ajue hata namna tu ya kufunga mahesabu ya biashara yake,” anasema.
Anatoa ushauri kwa kusema: “Mzazi anatakiwa kujua mtoto wake anapenda kufanya nini mapema kabla hata hajamaliza masomo yake. Kile anachopenda ndicho aendelezwe kwa gharama yoyote.”
Mwalimu mstaafu Erick Kimbe anasema wapo wanafunzi waliofeli kwa bahati mbaya kutokana na sababu mbalimbali, hata hivyo, wanaweza kufaulu ikiwa watapewa nafasi ya kurudia mitihani hiyo.
Anasema hakuna sababu kwa mzazi kukata tamaa na kuamua kumwacha mtoto wake nyumbani bila kazi yoyote, badala yake azungumze naye ajue masomo gani anaweza kufaulu kama akipewa nafasi ya kurudia.
“Ipo mifano ya watu wengi waliorudia mitihani na kufaulu, ingawa baadhi ya ndugu na jamaa zao waliwaona hawana akili kwa sababu tu walifeli mara ya kwanza,” anasema na kuongeza:
“Hakuna mtoto asiyeweza kila kitu, lazima kuna kitu anakimudu vyema tena wakati mwingine kuliko hata hao wanaoonekana kama wana akili darasani.”
Ni vyema kukumbuka kuwa watoto wengi wanafeli kwa sababu wazazi wao hawana muda wa kutosha kufuatilia maendeleo ya watoto wa shuleni. Mzazi au mlezi lazima akubali kuwa yeye ni sehemu ya matokeo mabaya anayoyapata mwanaye.
Wahenga walisema kuteleza siyo kuanguka, hivyo basi mshike mkono mwanao, jipange upya, nafasi ya kurekebisha makosa na kusonga mbele ni kubwa kinachotakiwa ni kuamini kuwa kushindwa mara ya kwanza kunatoa nafasi ya kujipanga upya.
Historia inataja watu wengi wenye mafanikio makubwa duniani ambao walianza kwa kushindwa, lakini baadaye walifanikiwa katika yale waliyokusudia.
Baadhi yao walishindwa zaidi ya mara moja lakini hawakukata tamaa, walitiwa moyo na ndugu na jamaa waliowazunguka.
Tajiri Bill Gates alipofungua kampuni yake ya kwanza ya Tra-O-Data alishindwa na kuamua kuifunga, Mwanahisabati maarufu, Isaac Newton ana historia ya kushindwa kulihudumia shamba la familia yao.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa