Home » » BAJETI NISHATI NA MADINI:MUHONGO AIITA NI YA MASINI

BAJETI NISHATI NA MADINI:MUHONGO AIITA NI YA MASINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amewasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka ujao wa fedha wa 2014/2015 ya shilingi trilioni 1.082 huku kati ya fedha hizo sh. bilioni 957.1 zikiwa ni fedha za miradi ya maendeleo na sh. bilioni 125.3 ikitengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida.

Profesa Muhongo amesema bajeti ya mwaka wa fedha wa 2014/2015 inakusudia kuimarisha na kuendeleza sekta za nishati na madini ili kuongeza mchango wake katika kujenga uchumi imara wa Taifa utakaotoa ajira mpya kwa Watanzania na kupunguza umaskini nchini.

Akiwasilisha hotuba ya Wizara hiyo bungeni mjini Dodoma jana, Profesa Muhongo alisema bajeti ya mwaka huu imelenga kuwainua maskini na kusisitiza kuwa Wizara hiyo ni ya miradi na sio mipango hivyo wananchi ni vyema kuchangamkia fursa zilizopo kunufaika.

Aidha Profesa Muhongo alisisitiza kauli yake kuwa hakutakuwa na mgawo wa umeme kutokana na wizara hiyo kujipanga vilivyo na kwamba kama utatokea mgawo basi ni wa magazetini na kwenye mitandao na si vinginevyo.

Sera na Sheria katika Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia

Alisema Serikali iliidhinisha Sera ya Gesi Asilia mwezi Oktoba, 2013 ili kuimarisha usimamizi wa Sekta Ndogo ya Gesi Asilia ambapo Rasimu ya Sera ya Uwezeshaji na Ushirikishaji Wazawa (Local Content Policy) ziliandaliwa.

Alisema lengo la sera hiyo ni kuhakikisha kuwa Watanzania wanashiriki ipasavyo katika shughuli zote za rasilimali za mafuta na gesi asilia kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vijavyo.

"Rasimu ya Sera hiyo imesambazwa kwa wadau mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, Wizara, Taasisi za Serikali na Washirika wa Maendeleo ili kupata maoni yao. Wizara ingependa kupata maoni yenu kabla ya tarehe 30 Juni, 2014,"alisema Profesa Muhongo.

Pia alisema Serikali imekamilisha Rasimu ya Kwanza ya Sera ya Petroli itakayotoa mwongozo kuhusu usimamizi wa shughuli za utafutaji, uzalishaji na ugawanaji mapato yanayotokana na Mafuta na Gesi Asilia pamoja na usafishaji, uhifadhi, usafirishaji na usambazaji mafuta.

Alisema katika mwaka 2014/15 Rasimu hizo zitawasilishwa katika Mamlaka husika kwa ajili ya kuidhinishwa ambapo kukamilika kwa sera husika kutaimarisha usimamizi wa Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia kwa maendeleo ya kizazi cha sasa na vijavyo.

"Mheshimiwa Spika, napenda kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa rasimu ya sheria ya gesi asilia imekamilika. Rasimu imepelekwa kwa wadau ili kupata maoni yao kabla ya kuikamilisha na kuiwasilisha katika kikao cha Bunge cha mwezi Novemba, 2014," alisema Profesa Muhongo.

Kuendeleza Shughuli za Uchimbaji Mdogo wa Madini

Ali s ema kat i k a mwaka 2013/14, shughuli za uchimbaji mdogo zimeendelea kukua na kutoa mchango mkubwa katika kupunguza umaskini, ambapo zaidi ya Watanzania milioni moja wamejiajiri katika shughuli hizo.

Hata hivyo katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 - 2015, Ibara ya 56 (d) ambayo pamoja na mambo mengine, inasisitiza juu ya kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata mikopo na mitaji, Wizara imeendelea kutoa mikopo ya masharti nafuu na ruzuku kwa wachimbaji wadogo kupitia Benki ya TIB.

Alisema mwezi Aprili, 2014 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alikabidhi hundi zenye jumla ya dola za Marekani 537,000 sawa na shilingi milioni 880.68 kwa miradi kumi na moja (11) ya wachimbaji wadogo ambayo ilikidhi vigezo vya kupata ruzuku.

Pia Wizara inatarajia kuipatia miradi mingine 18 ya wachimbaji wadogo mikopo yenye jumla ya shilingi bilioni 2.3 ifikapo mwishoni mwa mwezi Juni, 2014.

"Nawasihi wachimbaji wadogo kuandaa michanganuo yao ya miradi kwa ajili ya kuomba mikopo na ruzuku kupitia TIB ili watakaokidhi vigezo wapate ruzuku ama mikopo kwa ajili ya kuendesha shughuli zao za uchimbaji mdogo kwa tija. Wachimbaji wadogo wanashauriwa kupata ushauri wa bure wa kitaalamu kutoka Shirika la Taifa la Madini (STAMICO),"alisema.

Hata hivyo aliongeza kuwa wizara itaendelea kushirikiana kwa karibu sana na wachimbaji wadogo waaminifu watakaotumia vizuri ruzuku wanazopewa na watakaorejesha mikopo na kulipa kodi za Serikali.

Alisema ili kuendelea kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa mitaji na mikopo, Wizara imetenga kiasi cha sh. bilioni 2.5 katika Bajeti yake ya mwaka 2014/15 kwa ajili ya kukopesha wachimbaji hao.

Aidha katika juhudi za kuendeleza shughuli za uchimbaji mdogo, kwa mwaka 2013/14 wizara iliendelea kutoa mafunzo kwa nadharia na vitendo kwa wachimbaji wadogo ambapo jumla ya wachimbaji wadogo 420 walipatiwa mafunzo katika maeneo ya Handeni na Kilindi (250), Musoma (90) na Tunduru (80).

Aliongeza kuwa katika mwaka 2013/14 jumla ya maeneo 10 yenye ukubwa wa hekta 67,677.61 yametengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Maeneo hayo ni Nyamwironge (Kakonko), Ibaga (Mkalama), Makanya (Same), Mwajanga (Simanjiro), Itumbi B na Saza (Chunya), Ilujamate (Misungwi), Kalela/Kigogwe/ Samwa (mpakani mwa Wilaya za Kasulu, Buhigwe na Kigoma Vijijini), Maguja (Nachingwea) na Nyangalata (Kahama/ Nyang'hwale).

Pia jumla ya maeneo yaliyotengwa hadi sasa kwa ajili ya wachimbaji wadogo ni 25 yenye ukubwa wa kilomita za mraba 2,166.24. Aidha, jumla ya viwanja 8,800 vyenye ukubwa wa jumla ya kilomita za mraba 2,047.14 vimegawiwa kwa wachimbaji wadogo.

"Katika mwaka 2014/15, wizara itaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo kadri itakavyoonekana inafaa pamoja na kuongeza ajira kwa wachimbaji wadogo, utengaji wa maeneo unalenga kupunguza migogoro ya maeneo kati ya wachimbaji wadogo na wakubwa,"alisema.

Waziri Muhongo aliwashukuru viongozi wote wa dini nchini kwa kukubali kushirikiana na Wizara ya Nishati na Madini katika kuelimisha jamii kwa kauli mbiu isemayo "Uendelezaji wa Rasilimali za Gesi Asilia, Mafuta na Madini kwa Amani na Maendeleo ya Nchi Yetu."

Alisema kupitia viongozi hao wizara imeendelea kuelimisha jamii juu ya rasilimali zake katika makongamano mbalimbali nchini ambapo alivishukuru vyombo vya habari na wadau wengine kwa kushirikiana na Wizara ya Nishati na Madini katika kutoa habari na kuelimisha wananchi juu ya uendelezaji wa rasilimali zetu kwa manufaa ya Taifa.

"Nawaomba viongozi wa dini na wadau wengine tuendelee kushirikiana ili kuleta maendeleo endelevu kupitia rasilimali za nishati na madini. Napenda kuwahakikishia kuwa Wizara ya Nishati na Madini haitarudi nyuma katika kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto mbalimbali zinazoikabili na itaendelea kushirikisha jamii na wananchi kwa ujumla katika hatua zake za utekelezaji,"alisema Profesa Muhongo.

Chanzo;Majira


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa