Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Msuguano mkali umekuwa wakati Bunge linapokaa kama kamati 
kupitia vifungu vya bajeti za wizara husika. Hata hivyo, bajeti hizo 
zimepitishwa baada ya maelezo marefu na wakati mwingine msaada wa kiti 
cha Spika au pale Waziri Mkuu au Kaimu wake ndani ya Bunge anaposimama 
‘kuokoa jahazi’.
Mawaziri ambao hadi sasa wameingia katika orodha 
ya bajeti zao kupita kwa mbinde na wizara zao kwenye mabano ni Profesa 
Jumanne Maghembe (Maji), Profesa Anna Tibaijuka (Ardhi, Nyumba na 
Maendeleo ya Makazi), Profesa Sospeter Muhongo (Nishati na Madini), Dk 
John Magufuli (Ujenzi), Dk Harrison Mwakyembe (Uchukuzi), Sophia Simba 
(Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto) na Dk Seif Rashid
(Afya na Ustawi wa Jamii).
Sababu za kasheshe
Kwa sehemu kubwa, bajeti nyingi zilipata upinzani 
kutokana na Hazina kutoa fedha kidogo za maendeleo kati ya asilimia 19 
na 30 tu, wakati wizara nyingine zilitikiswa na tuhuma za ufisadi wa 
watendaji wake.
Sophia Simba
Miongoni mwa mivutano ni ule uliohusu taasisi ya 
Wanawake na Maendeleo (Wama) ambayo Mwenyekiti wake ni mke wa Rais 
Jakaya Kikwete, Mama Salma, hoja iliyoibuka wakati wa mjadala wa Bajeti 
ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto.
Mbunge wa Ole (CUF), Rajab Mbarouk Mohamed alitaka
 taasisi hiyo ifutwe, kwa maelezo kwamba inajihusisha na masuala ya 
kisiasa na kwamba mwaka 2010, Mama Salma aliitumia kumfanyia kampeni 
mumewe.
Katika hoja hiyo alisema mmoja wa wajumbe wa bodi 
ya taasisi hiyo ni Waziri wa wizara hiyo, Sophia Simba kinyume na sheria
 na taratibu.
Waziri Simba akajibu: “Nipo Wama lakini kazi 
ninayoifanya pale ni ya kujitolea na silipwi kitu. Kanuni na sheria 
zinakataza mtu kujihusisha na taasisi nyingine kama tu anakuwa analipwa 
mshahara”.
Profesa Maghembe
Juzi, Profesa Maghembe alipata wakati mgumu baada 
ya hoja iliyoshika mshahara wake iliyotolewa na Mbunge wa Ubungo 
(Chadema), John Mnyika kujadiliwa kwa dakika 31, hadi Kaimu Waziri Mkuu,
 Profesa Mark Mwandosya alipoingilia kati.
Wabunge bila kujali itikadi za vyama vyao, waliungana kutetea 
hoja ya kutaka suala la upatikanaji wa maji liwe ajenda ya kwanza ya 
Serikali. mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Pauline Gekul alitaka bajeti
 hiyo ifumuliwe ili kuondoa posho za vikao na safari.
Mbunge wa Lushoto (CCM), Henry Shekifu alisema tatizo la maji ni zito na akapendekeza kuanzishwa kwa mfuko wa maji.
Profesa Mwandosya alisimama na kutoa uthibitisho 
kwa niaba ya Serikali kwamba muswada huo wa fedha utapelekwa bungeni 
kabla ya kuvunjwa kwa Bunge 2015 na alikubaliana na wabunge kwamba suala
 la maji litakuwa ni nambari moja katika vipaumbele vya Serikali.
Dk Magufuli
Kauli ya Waziri wa Ujenzi, Dk Magufuli kwamba 
ujenzi wa barabara si sawa na chapati, ilisababisha baadhi ya wabunge 
kumjia juu wakati wa kupitisha vifungu vya bajeti ya wizara yake.
Baadhi ya wabunge wa mikoa ya kusini mwa nchi, 
walichachamaa kutokana kile walichodai kuwa ni kutotengwa kwa fedha za 
ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami.
Suala jingine lililotawala mjadala huo ni sakata 
la malori kuruhusiwa kuzidisha uzito barabarani, hoja ambayo iliibuliwa 
na Machali ambaye alimtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwaomba radhi 
Watanzania kutokana na hatua yake ya kuyaruhusu kubeba mizigo mizito na 
kusababisha barabara zinazojengwa kwa mamilioni ya fedha za kodi za 
wananchi kuharibika. Pinda alitoa ufafanuzi mzuri.
Dk Mwakyembe
Wabunge walitaka maelezo ya kina juu ya 
uendeleshaji Shirika la Usafiri Dar es Salaam (Uda), Shirika la Ndege 
(ATCL), ukarabati wa meli ya MV Victoria na upanuzi uwanja wa ndege 
Mwanza.
Wabunge waliokuwa vinara wa kupinga bajeti hiyo 
wakitaka mambo hayo manne kupatiwa ufumbuzi ni wabunge wa CCM, Dk Hamisi
 Kigwangalla (Nzega), Andrew Chenge (Bariadi Magharibi), Charles Mwijage
 (Muleba Kaskazini), Richard Ndassa(Sumve) na mbunge wa Ilemela 
(Chadema), Ezekiah Wenje.
Profesa Muhongo
Ni kati ya bajeti ambazo zilipita kwa mbinde huku wabunge wakiibua hoja na ufisadi mbalimbali uliofanywa ndani ya wizara hiyo.
Sakata la IPTL ni moja kati ya mambo yaliyotikisa mjadala wa 
bajeti hiyo huku Mnyika na mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole 
Sendeka wakiwasilisha ushahidi kuhusu tuhuma kadhaa za wizara hiyo.
Mashambulizi hayo yaliibua tuhuma mpya dhidi ya 
wabunge, Profesa Muhongo alipodai kwamba baadhi ya wabunge wakiwamo wa 
upinzani wamehongwa na IPTL.
Katika maelezo yake, Profesa Muhongo alisema ana 
ushahidi wa kamera za CCTV zinazowaonyesha vigogo hao wa upinzani 
wakisaini nyaraka na kuchukua fedha hizo.
Sakata jingine lililoibuka ni kukosekana kwa umeme
 katika maeneo ya vijijini na kulazimika Waziri Mkuu, Mizengo Pinda 
kutoa ufafanuzi akisema kuwa fedha zitakazotengwa kwa ajili ya Mfuko wa 
Nishati Vijijini (Rea) hazitaguswa.
Profesa Tibaijuka
Waziri Tibaijuka alijikuta katika wakati mgumu 
baada ya wabunge, wengi wa Dar es Salaam kumbana kuhusu ujenzi wa mji 
mpya wa Kigamboni.
Suala hilo lililohusishwa na ufisadi lilionekana 
kumchanganya waziri huyo na wakati mwingine alishindwa kujibu maswali na
 badala yake kuwashambulia wabunge wa upinzani hasa Halima Mdee wa 
Chadema.
Alisema wapo wabunge ambao walikuwa na hoja na 
wengine walikuwa wakipiga kelele, akitoa mfano tuhuma dhidi yake kuwa 
anamiliki kiwanja katika Mji wa Kigamboni kwamba hazina ukweli wowote.
Dk Seif Rashid
Nayo Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ilikumbwa 
na dhoruba jana kabla ya kuokolewa na Profesa Mwandosya baada ya wabunge
 wengi hususan wanawake, kutaka kuikwamisha.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment