Home » » Albino 43 wauawa nchini.

Albino 43 wauawa nchini.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Waziri mkuu, Mizengo Pinda.
Watu 43 wenye ulemavu wa ngozi wameuawa, huku watuhumiwa 13 wamehukumiwa kunyongwa hadi kufa baada ya kupatikana na hatia ya mauaji ya watu hao.
 
Waziri mkuu, Mizengo Pinda, aliliambia Bunge jana wakati akiwasilisha hotuba ya muelekeo wa kazi za Serikali, makadirio ya matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Bunge kwa mwaka 2015/16 kuwa, mauaji hayo yamesababisha hofu kwa watu wenye ulemavu wa ngozi pamoja na familia zao kuishi kwa hofu, mashaka na kushindwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo. 
 
“Vitendo hivi vimeleta taswira isiyo nzuri kwa nchi yetu ikizingatiwa kwamba watu wengi ndani na nje ya nchi wanafahamu kuwa Watanzania wanaishi kwa upendo, kuheshimiana na kuthamini amani, jambo ambalo nchi nyingi zinaendelea kuiga,” alisema. 
 
Alisema tangu mauaji hayo yalipoanza mwaka 2006, watuhumiwa 181 walikamatwa na kuhojiwa na kwamba kati ya yao 131 walifikishwa mahakamani, ambapo 46 walifunguliwa kesi za kuua na kujeruhi na kwamba kati yao washtakiwa  13 wamehukumiwa kifo. 
 
Aidha, mshtakiwa mmoja alihukumiwa kifungo cha miaka 20 kwa hatia ya kujeruhi, wakati wengine 73 wameachiwa huru  baada ya kukosekana ushahidi wa kuwatia hatiani.  
 
Kutokana na hali hiyo, Pinda alisema kuanzia mwaka 2006 hadi sasa watu 43 wenye ulemavu wa ngozi wameuawa, huku mwaka huu pekee wakiwa wameuawa watu tisa.  
 
Alisema watuhumiwa sita hawajakamatwa na upelelezi wa kesi 10 bado unaendelea, huku watuhumiwa wawili wakiuawa na wananchi kabla ya kufikishwa polisi. Pinda alisema chanzo kikubwa cha mauaji hayo ni imani za kishirikina kwa tamaa za kupata utajiri au chezo. “Mimi siamini kwamba cheo, wadhifa, mali au utajiri hupatikana kwa njia haramu kama hizo. 
 
Utajiri hupatikana kwa kufanyakazi kwa juhudi na maarifa na siyo vinginevyo…serikali itaendelea kupambana na watu wanaojihusisha na vitendo hivyo kwa nguvu zake zote,” alisema. Awali, akizungumza bungeni kabla ya kutoa hutuba, Pinda alisema Kanda ya Ziwa inaongoza kwa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi, ambapo kati ya watu 43 waliouawa 41 wametoka katika kanda hiyo. 
 
Ufafanuzi huo alitoa wakati alipokuwa akitoa majibu ya ziada katika swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum, Martha Umbulla (CCM), ambaye alitaka kujua sababu  za mauaji ya albino kuendelea licha ya kwamba kumekuwa na juhudi za kukomesha vitendo hivyo. 
 
Alisema ili kuelimisha na kuhamasisha wananchi wa mikoa hiyo ikiwamo Mwanza, Geita, Simiyu, Shinyanga, Kagera na  Mara kuacha imani hizo za kishirikina, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala  Bora (CHRAGG)  pamoja na  viongozi wa dini watatembelea na kuhamasisha wananchi wa ameneo hayo kubadili tabia. Aliliambia Bunge kuwa  tume hiyo ya haki za binadamu na madhehebu ya dini yatatembelea kanda hiyo  na kuzungumza na wananchi na kutoa elimu inayolenga kuleta mabadiliko. Alisema serikali ina amini kuwa kampeni hiyo pamoja kazi za mahakama itapunguza mauaji ya albino nchini. 
 
Vitendo vya kuwakata viungo albino vilianza 2006 kwa imani potofu kuwa ni chanzo cha utajiri , mafanikio kisiasa na kiuchumi. Baadhi wanaamini kuwa vinasaidia kupanda vyeo na kufanikiwa kazini.   
 
BVR
Alisema  matumizi ya mfumo wa kisasa wa Biometric Voters Registration (BVR) katika maboresho ya Daftari la Kudumu la Wapira Kura ulioanza Februari 23, mwaka huu, hautatumika kwa ajili ya kupiga au kuhesabu kura. 
 
"Napenda kulikumbusha Bunge lako na wananchi wote kwamba, Tanzania itatumia mfumo wa BVR kwa ajili ya uandikishaji tu na hautatumika kwa ajili ya kupiga au kuhesabu kura kama wengine wanavyoamini. 
 
Hata hivyo, hakutoa sababu za kutotumia mfumo huo katika kupiga au kuhesabu kura. “Wale wote wenye sifa watapiga kura kwa utaratibu wa kawaida wa kutumia karatasi maalum na matokeo yatatolewa na kubandikwa vituoni kama ambavyo imekuwa ikifanyika kwenye chaguzi zilizopita.” 
 
“Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaendelea kutoa elimu, taarifa na ratiba kwa umma kuhusu zoezi la uandikishaji linavyofanyika katika maeneo yote nchini,” alisema. Alisema Nec imeanza maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 pamoja na maandalizi ya kupiga kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa.  
 
HALI YA SIASA 
Akizungumzia hali ya siasa nchini, alisema imeendelea kuimarika, demokrasia imeendelea kukua na mwamko wa wananchi kushiriki katika shughuli za siasa umeongezeka. Alisema idadi ya vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu imeongezeka kutoka 17 mwaka 2005/06 hadi 22 mwaka 2014/15. Aidha, alisema hadi kufikia Februari, 2015, vyama vingine nane vimewasilisha maombi ya usajili wa muda.  
 
KESI 10 KUBWA ZA RUSHWA  
Kuhusu mapambano dhidi ya rushwa, Pinda alisema Taasisi ya Kupambana na Kudhibiti Rushwa (Takukuru) inatakiwa kukamilisha uchunguzi wa tuhuma 10 za rushwa kubwa, kuchunguza tuhuma 2,783 zilizopo na mpya zitakazojitokeza 2015/16.   
 
KERO ZA MUUNGANO 
Pinda alisema kero 15 za Muungano zinajadiliwa na Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ). 
 
Alisema kati ya hoja hizo, tisa zimepatiwa ufumbuzi na sita zipo katika hatua ya utatuzi. 
 
Alizitaja hoja zilizo katika hatua ya utatuzi kuwa ni mgawanyo wa mapato ambaio inajumuisha mgawo wa misaada kutoka nchi za nje na misamaha ya mikopo. 
 
Nyingine ni hisa za SMZ zilizokuwa katika Bodi ya  Sarafu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na faida ya Benki Kuu.  Alitaja nyingine kuwa ni utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia, ushiriki wa Zanzibar katika taasisi za nje, ajira za Zanzibar katika taasisi za Muungano, usajili wa vyombo vya moto na Tume ya Pamoja ya Fedha. Alisema ni dhamira ya serikali mbili hizo kuzipatia ufumbuzi hoja hizo haraka inavyowezekana.  
 
UJENZI BANDARI MPYA Alisema ujenzi wa bandari kubwa kuliko zote ukanda wa Afrika Mashariki na kati unatarajiwa kuanza 2015/16, eneo la Mbegani, wilayani Bagamoyo.  
 
NISHATI Waziri Mkuu Pinda alisema, serikali imekamilisha kwa asilimia 84 utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi wa kufua umeme wa Kinyerezi utakaozalisha megawati 150 kwa kutumia gesi asilia. Alisema utekelezaji wa awamu ya tatu ya mradi huo utakaozalisha megawati 300 unaendelea.  
 
GESI ASILIA 
Alisema ugunduzi wa kiasi kikubwa cha gesi asilia nchini umeiweka Tanzania katika orodha ya nchi zinazozalisha gesi asilia nyingi duniani na kutoa matumaini makubwa ya kukuza uchumi. Alisema hadi kufika Desemba, mwaka jana, gesi asilia yenye futi za ujazo trilioni 53.28 ilikuwa imegunduliwa na kazi ya utafutaji inaendelea.  
 
Imeandikwa na Jacqueline Massano,  Gaudencia Mngumi na John Ngunge, Dodoma
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa