Home » » MKOA WA DODOMA KUANDAA KONGAMANO LA UWEKEZAJI.‏

MKOA WA DODOMA KUANDAA KONGAMANO LA UWEKEZAJI.‏

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Na Mwandishi,Dodoma.
Mkoa wa Dodoma unakusudia kuandaa kongamano la kuzitangaza fursa zilizopo katika mkoa huu baadae mwakani ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje kuja kuwekeza na kukuza uchimi na kuongeza kipato cha wananchi wake.
Hayo yalielezwa jana hapa mjini Dodoma na mchumi wa kamati ya maendeleo ya mkoa, Bwana Paulo Ngussa alipokuwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake. Alisema, mkoa wetu wa Dodoma inazo fursa nyingi ambazo bado hazijapata wawekezaji hivyo kamati ya maendeleo ya mkoa huu kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa imekusudia kuandaa kongamano hilo litakalofanyika mwanzoni mwa mwezi wa nane.
Alizita baadhi ya fursa hizo kuwa ni uwekezaji katika sekta ya kilimo na mifugo ambapo alitaja ukulima wa zabibu na ngozi toka machinjio ya Dodoma yanayozalisha ngozi za kutosha kibiashara. Alisema kwa sasa zabibu zinalimwa hapa Dodoma lakini hakuna soko la uhakika hivyo wangependa apatikane mwekezaji wa kujenga kiwanda cha kutengeneza juisi au wani. Alienda mbali kidogo katika sekta ya kilimo kwa kubainisha kuwa, mkoa huu wa Dodoma mvua zake ni chache sana na karibuni kipindi cha miezi tisa ni ukame na watu wake hukaa bila shughuli za kufanya. Mkoa unakusudia wapatikane wawekezaji katika mpango wa umwagiliaji ili wananchi wake waweze kujishughulisha na kilimo cha umwagiliaji mfano mbogamboga nk.
Alitaja eneo jingi kuwa ni sekta ya elimu ambapo mkoa wa Dodoma unao vyuo vingi vya elimu ya juu lakini lipo tatizo kubwa la hosteli za wanafunzi na nyumba za watumishi. Kwa sasa nyumba zilizopo Dodoma ni zile za asili ambazo haziwezi kukidhi haja ya jamii ya sasa, alieleza mchumi huyo.
Pia eneo jingine ni la sekta ya utalii ambapo hadi sasa Dodoma haina kumbi kubwa za kutosha za  mikutano ya kitaifa na kimataifa. Pia mkoa hauna hoteli kubwa za kiwango cha nyota tano. Alieleza kuwa pamoja na mkoa kuwa ni makao makuu tarajiwa ya nchi, na pia kufanyika kwa vikao vya bunge lakini lipo tatizo kuwa la kumbi za mikutano kwa viongozi na watendaji wa serikali. “Wageni wanaotaka kuja kuwaona viongozo Dodoma lazima wavizie wakati wa shughuli za bunge na kurejea Dar es Salaam”, alifafanua hivyo.
Alimalizia kwa kutaja pia sekta ya madini ambayo inakuwa kwa kasi hapa nchini. Maeneo ya milima ya Mpwawa yamegundulika kuwa na aina mbalimbali za madini lakini bado fursa hiyo haija tangazwa vya kutosha.
Kulingana na takwimu za mwaka 2013 za kipato cha mtu mmoja mmoja kwa  mkoa wa Dodoma ni shilingi 757,696.00 kwa mwaka, ambapo mikoa mingine mfano Dar es Salaam ni zaidi ya milioni moja. Imeelezwa pia kuwa maadalizi hayo yanatarajiwa kugharamiwa na wadau wote wa maendeleo hapa mkoani na inakadiriwa kiasi cha shilingi milioni mia nane kufanikisha kongamano hilo.

    

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa