Home » » UHAMIAJI WACHUKUA HATUA KUONDOA RUSHWA

UHAMIAJI WACHUKUA HATUA KUONDOA RUSHWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Imeandikwa na Stella Nyemenohi, Dodoma
IDARA ya Uhamiaji imekiri kuwapo upotevu wa mapato kwenye kitengo cha utoaji viza katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam.
Imesema ili kukabiliana na hali hiyo pamoja na mambo mengine imeanzisha huduma za kimtandao.

 Aidha, baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) wametuhumu idara katika uwanja huo wa ndege kugubikwa na rushwa jambo ambalo limekuwa likisababisha usumbufu kwa wageni wanaoingia na kutoka nchini kwa kuwacheleweshea au kuwazungusha kupata huduma.

Hayo yalibainishwa jana kwenye kikao cha PAC na watendaji wa idara hiyo wakiongozwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Projest Rwegasira, waliokiri kuwapo upotevu wa mapato yatokanayo na malipo ya viza ambao tayari umetafutiwa utatuzi. “Kwenye suala la viza ni kweli fedha nyingi zimekuwa zikipotea,” alisema Kamishna wa Utawala na Fedha, Edward Chogero na kufafanua kuwa pamoja na hatua nyingine, wako kwenye mchakato wa kuanzisha mfumo wa viza mtandao.

Alikiri tatizo hilo na kusema wameanza mchakato wa kuhakikisha fedha hazipotei na pia wanadhibiti rushwa. Alisema ipo timu inayoundwa na wadau wote wakiwemo Wizara ya Fedha na Mipango, Uhamiaji, Usalama wa Taifa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa ajili ya kuboresha viza mtandao ili fedha ziwe zinaingia moja kwa moja serikali badala ya kuingia mikononi mwa watu .

Chogero alisema baada ya kuona mianya ya rushwa ikiwamo foleni katika JNIA, wameongeza madirisha ya malipo yawe 10 kiasi ambacho hakuna mtumishi anayeweza kuomba rushwa ili amhudumie mteja haraka. Kwa upande wa Uwanja wa Kimataifa wa Ndege Kilimanjaro (KIA), alisema kulikuwa na kompyuta tatu na wiki iliyopita wameongeza zimefika tisa.
“ Tunajaribu kuimarisha na tumepata fedha kutoka serikali, wakati tunaendelea kuimarisha mfumo, tutapata fedha kwa ajili ya vituo vilivyo mkoani.

 Hakuna mtu atagongewa muhuri tu bila kuwekewa stika,” alisema. Awali, katika hoja za wajumbe wa kamati kuhusu upotevu wa mapato, Mbunge wa Magomeni, Jamal Kassim (CCM) akinukuu taarifa ya ukaguzi ya CAG mwaka wa fedha 2015/2016 , alisema sampuli ya wageni 65 iliyochukuliwa JNIA, baada ya kufuatilia ilibainika kati yao, watu 20 taarifa zao za malipo ya viza hazikuwapo.

Akizungumzia rushwa, Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe (CCM) alisema JNIA umechafuka kwa vitendo hivyo vinavyofanywa kwa nguvu na baadhi ya watumishi dhidi ya wageni na kuwakatisha tamaa.

Kwa mujibu wa mbunge huyo, mgeni anaweza kuzungushwa au kuwekewa vikwazo katika kupatiwa huduma ili atoe rushwa. Alitoa mfano kuwa yupo jirani yake, ana mdogo yake anayechezea timu ya Simba, alipata wageni kutoka Ivory Coast ambao baada ya kufika, walitaka watokee nchini kwenda Vietnam, lakini waliwekewa vikwazo kwamba lazima warudi nchini kwao ndipo waende nchi hiyo.

CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa