Home » » DOKTA MPANGO AWASHAURI WAKANDARASI KUTUMIA MALIGHAFI ZA NDANI KATIKA SEKTA YA UJENZI

DOKTA MPANGO AWASHAURI WAKANDARASI KUTUMIA MALIGHAFI ZA NDANI KATIKA SEKTA YA UJENZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Benny Mwaipaja, Dodoma

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), amekagua ujenzi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu-NBS mjini Dodoma na kutoa wito kwa wakandarasi wanaojenga miundombinu mbalimbali yakiwemo majengo kutumia malighafi zinazozalishwa hapa nchini ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Amesema hayo baada ya kushuhudia mkandarasi anayejenga jengo hilo Hainan International Ltd ya China, akitumia vifaa mbalimbali vya ujenzi vinavyopatikana hapa nchini zikiwemo mbao na vifaa vya umeme, hatua ambayo amesema inachangia kuwaongezea kipato wananchi.

Akizungumzia ujenzi huo, Dkt. Mpango amesema jengo hilo litatumika ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa kwakuwa litatumika kuchakata takwimu mbalimbali zitakazotumika katika kutunga sera na mipango mbalimbali ya kuendeleza nchi.

“Huwezi kupanga mipango yoyote bila kuwa na takwimu nzuri na bora, hapa ndipo vile “vichwa” vyetu vya takwimu nchini vitachakata takwimu hizo ndipo zitumike katika kutunga sera bora kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu” Alisistiza Dkt. Mpango

Dkt. Mpango alielezea furaha yake kwamba jengo hilo linajengwa mjini Dodoma badala ya Dar es Salaam ambako lilikuwa lijengwe ili kusukuma azma ya Serikali ya kuhamia Dodoma kwa kuhakikisha miundombinu muhimu zikiwemo ofisi vinapatikana.

Aidha, ameeleza kuwa ujenzi wa jengo hilo lenye ghorofa 5, umetoa ajira kwa zaidi ya vijana 120 kutoka sehemu mbalimbali nchini hatua ambayo amesema imewafanya vijana wengi kujipatia kipato cha kujikimu maisha yao.

Dkt. Mpango ameupongeza uongozi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), kwa kazi nzuri wanayoifanya ya ujenzi wa ofisi mpya katika Makao Makuu ya Nchi mjini Dodoma inayojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia, Umoja wa Ulaya, Mashirika ya Maendeleo ya Kimataifa ya Canada na Uingereza kwa kushirikiana na  Serikali.

Kwa upande wake Mtaalam Mshauri na Mdhibiti Viwango anayesimamia ujenzi wa jengo hilo Mhandisi Abdulkarim Msuya amesema kuwa jengo hilo lenye thamani
ya shilingi bilioni 11.6 linatarajiwa kukamilika mwezi Januari mwakani.

Amesema kuwa ujenzi huo umefikia hatua za mwisho kwa asilimia 82 ambapo asilimia 18 zilizobaki ni za umaliziaji na kwamba mkandarasi aliyepewa kazi hiyo anatarajia kukamilisha kazi hiyo ndani ya siku 30 hadi 45 kuanzia sasa.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa