Home » » WAPINZANI SASA KUIBUKA BUNGENI NA MIKAKATI MIPYA

WAPINZANI SASA KUIBUKA BUNGENI NA MIKAKATI MIPYA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu.
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, imejipanga kuibuka na mikakati mipya ndani ya Bunge linalotarajiwa kuanza mjini Dodoma Januari 27, mwaka huu.
 
Aidha, kambi hiyo imepanga kutangaza Baraza lake la  mawaziri kivuli Januari 26, mwaka huu.
 
Chanzo kutoka ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeliambia Nipashe kuwa siku hiyo atafahamika Mnadhimu wa kambi hiyo pamoja na mawaziri kivuli wa kambi hiyo.
 
Kambi hiyo inaundwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), inayojumuisha vyama vya Chadema ambacho ni chama kikuu cha upinzani Tanzania Bara, Chama cha Wananchi (CUF)ambacho ni chama kikuu cha upinzani Zanzibar, NLD na NCCR-Mageuzi.
 
Chanzo hicho kimeeleza kuwa mikakati ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa Bunge lijalo, itawekwa hadharani siku hiyo ikiwa ni pamoja na namna walivyojipanga katika kuweka hoja mbalimbali.
 
Aidha, imebainika kuwa Ukawa inajipanga kuja na muundo mpya kwa kuwanoa zaidi wabunge wao ili kuuonyesha umma namna walivyojiweka tayari kuendesha serikali.
 
“Moja ya mambo ambayo lazima tuonyeshe tofauti, ni jinsi tulivyokuwa tumejipanga kuongoza serikali ya awamu ya tano. Hivyo wabunge wetu wataonekana tofauti hasa katika uchangiaji na uwasilishaji wa hoja mbalimbali,” kilieleza chanzo hicho.
 
Kilisema hoja kubwa ambayo itatawala katika Bunge hilo ni hotuba ya Rais ambayo kambi hiyo imebaini kuwapo kwa mapungufu mengi.
 
“Mjadala wetu katika Bunge hili, utajikita katika hotuba ya Rais aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa Bunge Novemba, mwaka jana. Yapo mambo mengi yenye upungufu yanayohitaji serikali kutoa ufafanuzi,” alisema.
 
Aidha, chanzo hicho kimeeleza kuwa pamoja na muundo mpya wa utendaji kazi wa wabunge hao, suala la migomo ya kutoka nje pale wanapoona Bunge linaendeshwa ndivyo sivyo, litajitokeza kama ilivyokuwa katika mikutano ya Bunge iliyopita.
 
Kambi hiyo kwa sasa itaundwa na wabunge 113 wa upinzani, tofauti na Bunge la 10 waolikuwa 91.
 
Katika Bunge lililopita, Mnadhimu Mkuu wa Bunge alikuwa ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu.
 
Bunge la 10 lilitawaliwa na mvutano baina ya wabunge wa upinzani na wa CCM.
 
Mara kadhaa, wabunge wa upinzani walitoka nje wakati Bunge likiendelea kuonyesha kutokukubaliana na baadhi ya hoja.
 
Mathalani, walitoka wakati wa uwasilishwaji wa na kujadiliwa kwa miswada ya sheria za mafuta na gesi, mapato yatokanayo na mafuta na gesi.
 
Zomea zomea pia ilitawala katika bunge hilo, kiasi cha kiti cha Spika kushindwa kuendesha baadhi ya vikao na kulazimika kuahirisha kwa muda.
CHANZO: NIPASH.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa