Home » » DK.MPANGO: SITARUHUSU MISAMAHA YA KODIISIYO NA MASLAHI KWA TAIFA.

DK.MPANGO: SITARUHUSU MISAMAHA YA KODIISIYO NA MASLAHI KWA TAIFA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Waziri wa Fedha, Dk. Philip Mpango.
Waziri wa Fedha, Dk. Philip Mpango, amesema hatakubali kuruhusu misamaha ya kodi isiyokuwa na maslahi kwa taifa.
 
Alisema hayo jana bungeni wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge Viti Maalum (Chadema), Upendo Peneza, ambaye alisema ripoti hazionyeshi faida ambayo serikali inazipata kutokana na misamaha ya kodi, hasa kwenye kampuni za uwekezaji katika sekta ya madini.
 
“ je serikali  ina mpango gani wa kuhakikisha kampuni hizi zinaondolewa kwenye misamaha ya kodi na kuanza kulipa kodi ili wajibu wa kutoa huduma za jamii ubakie kwa serikali?,” alihoji Peneza.
 
Akijibu, Dk. Mpango alisema wizara yake imeongeza vitengo vya kukagua misamaha ya kodi ili kuhakikisha misamaha ya kodi itakayoruhusiwa ni ile tu yenye faida kwa taifa.
 
Alisema misamaha ya kodi ambayo imekuwa ikitolewa kwenye kampuni za madini imepungua kutoka takribani asilimia 17.6 ya kodi zote zinatolewa na kufikia asilimia tisa.
 
Alisema hatua zilizochukuliwa ni kurekebisha sheria za kodi na wabunge walipitisha marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongeleko la Thamani ambayo iliondoa misamaha mingi ya kodi.
 
Alisema misamaha ya kodi ni asilimia 56 ya mapato ya kodi zote na kwamba maboresho ya sheria hiyo ya misamaha ya kodi imesaidia kupungua kwa kiasi kikubwa tatizo hilo.
 
Aidha, Dk. Mpango alisema wanafanya jitihada kubwa kushughulikia mazingira ya biashara na uwekezaji, kwa kuwa uwekezaji hautegemee kodi peke yake.
 
Awali, akijibu swali la msingi la Mbunge huyo, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles  Mwijage, alisema misamaha ya kodi ni moja ya vivutio vinavyotolewa kuwahamasisha  wawekezaji  waichague Tanzania.
 
Hata hivyo, alisema serikali inatambua mapungufu  yaliyoko katika kutumia kodi kama kivutio cha uwekezaji.
 
“Tatizo kubwa ni wale wanaotumia fursa hii kuhujuma mapato ya serikali pale misamaha inaposababisha kutokuwapo na ushindani sawa kati ya kampuni moja na nyingine, lakini serikali itaendelea kufanya maboresho ya sheria  ili kupunguza misamaha ya kodi,” aliongeza kusema.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa