Masoud Masasi, Dodoma Yetu
ZOEZI la sense mkoani Dodoma limeanza kutia dosari baada ya jana kuibuka vurugu katika kata ya Hogolo, Tarafa ya Zoisa, Wilayani Kongwa,kutokana na baadhi ya wakazi wa kata hiyo kugoma kuhesabiwa hadi hapo waganga wa kienyeji maarufu kama “lambalamba’ wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani hapa watakapoachiwa huru.
Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Alfred Msovella, alieleza kuwa kikundi hicho kinachofanya shughuli zisizo rasmi za kuwabaini watu wanaojihusisha na ushirikina kilizuiwa na serikali kufanya sghuli hizo lakini wakazi wa kata hiyo wamekuwa wakihamasisha kuwa lazima kikundi hicho kiruhusiwe ndipo waweze kuhesabiwa.
Msovella alisema kuwa, juzi wakazi hao walifunga barabara kama ishara kukataa kuhesabiwa jambo ambalo lilifanya magari kushindwa kupita.
Alisema kutokana na hali hiyo waliamua kupeleka polisi kwa madhumuni ya kulinda usalama lakini hawakuweza kumudu jambo ambalo liliwalazimu kuomba nguvu mkoani na walifanikiwa kuletewa askari wa kutuliza
ghasia (F.F.U).
Alifafanua kuwa polisi ililazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi hao ambao walikuwa wakiapa kuwa hawatahesabiwa hadi hapo lambalamba wataachiwa huru na kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao za uganga.
Msovella alisema jana hali hiyo ilijirudia ambapo kundi kubwa la vijana walifunga barabara kwa magogo wakipinga kuhesabiwa hadi hapo lambalamba watakapoachiwa huru.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma Zelothe Stephen alisema yeye binafsi si msemaji wa masuala ya sensa lakini Polisi hawawezi kuwaachia waganga hao kuendelea kufanya shughuli hizo.
Alisisitiza kuwa, wao kama Jeshi la Polisi wata mkamata mtu yeyote ambaye atajifanya mganga katika eneo hilo na lingine lolote ili kuhakikisha amani inakuwepo.
Aidha mkuu Mkoa wa Dodoma Dk. Rehema Nchimbi alisema Serikali imepata taarifa hiyo na haiwezi kumuachia mtu yeyote mwenye makosa kwa shinikizo la watu.
Alisema sensa haina uhusiano wowote na masuala ya ushirikina hivyo yeyote atakayebainika kuharibu zoezi hilo atachukuliwa hatua za kisheria.
Blogzamikoa
0 comments:
Post a Comment