Home »
» Mbunge Nassari afichua siri nzito
Mbunge Nassari afichua siri nzito
Mbunge
wa Arumeru Mashariki, Bw. Joshua Nassari (CHADEMA), amesema Mbunge wa
Arusha Mjini kwa tiketi ya chama hicho, Bw. Godbless Lema yupo katika
hatari ya kubambikiwa kesi.
Alisema ipo mipango inayosukwa ili
kumhusisha Bw. Lema na milipuko ya mabomu katika mikutano ya chama
hicho, eneo la Soweto na ule wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph
Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, mkoani humo.
Bw. Nassari aliyasema
hayo bungeni Mjini Dodoma jana katika kipindi cha maswali kwa Waziri
Mkuu, Bw. Mizengo Pinda na kuongeza kuwa ni wajibu wa Serikali kusimamia
haki badala ya kuwabambikia kesi wanasiasa kwa lengo la kudhoofisha
vyama vya upinzani.
Alisema kwa mara kadhaa, amewahi kutembelea
magereza na kujionea vijana wengi wakiwa ndani bila hatia na kutolea
mfano wa kijana ambaye alikamatwa na kuwekwa mahabusu akihusishwa na
ulipuaji wa bomu Soweto na Olasiti.
"Huyu kijana yupo tayari kutoa
ushahidi...alikamatwa Arusha na kupelekwa Mwanza, baadaye alihamishiwa
mkoani Shinyanga ambako aliminywa sehemu zake za siri na kuvunjwa mguu
ili amtaje Lema kuwa alihusika na matukio hayo," alisema.
Bw.
Nassari alimtaka Bw. Pinda kutoa ufafanuzi juu ya Serikali
kuwabambikizia watu kesi ili kuvidhoofisha vyama vya upinzani badala ya
kusimamia upatikanaji wa haki kwa raia wake.
Akijibu swali hilo, Bw.
Pinda alisema si nia ya Serikali kutaka kuwabambikizia watu kesi ambapo
mambo yaliyotokea Soweto na Olasiti si madogo na yeye hana taarifa za
suala hilo.
Alisema Serikali inaendelea na uchunguzi ili kuwabaini watu waliohusika na milipuko hiyo na
kama kuna Mbunge anayejua kila kitu ni vyema akatoa taarifa hizo ili ziweze kupelekwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
"Kwa
kweli siwezi kujibu swali hilo...Mheshimiwa Nassari anajua kila kitu na
mimi sina taarifa lakini si nia ya Serikali kuwabambikizia watu kesi ni
vyema uandike maelezo yako kwa maandishi ili niwape wahusika ambao ni
Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi wachunguze," alisema.
Kwa upande
wake, Bw. Lema alisema amekuwa na wasiwasi juu ya suala hilo kwani yeye
hausiki na jambo hilo na mhusika yupo ambaye alilazimishwa ili amtaje
yeye.
Chanzo;Majira
0 comments:
Post a Comment