Home » » Hatutakubali kuburuzwa bungeni

Hatutakubali kuburuzwa bungeni

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ni moja ya makundi ambayo yamekuwa na sauti kubwa katika Bunge la Katiba linaloendelea mjini Dodoma.
Umoja huu unaundwa na wajumbe kutoka vyama vya upinzani na baadhi ya wawakilishi wa makundi yaliyoteuliwa na Rais Jakaya Kikwete na baadhi ya wabunge wa CCM.
Julius Mtatilo ni katibu wa muda wa kundi hilo. Katika mahojiano maalumu na Mwananchi, Mtatiro anaeleza mambo kadhaa yanayohusu umoja huo kama ifuatavyo;
Swali: Katika siku za karibuni Ukawa ni moja ya makundi ambayo yamekuwa yakitajwa sana kwenye Mchakato wa Katiba Mpya. Je, nini maana yake na ulianza lini?
Jibu: Ukawa ni kifupi cha Umoja wa Kutetea Hoja za Wananchi zilizopo kwenye Rasimu ya Katiba ambayo imewasilishwa bungeni na Jaji Joseph Warioba.
Swali: Umoja huu umeanzishwa lini na kwanini ulianzishwa?
Jibu: Ukawa ulianzishwa mara tu baada ya kufika bungeni na kuona wenzetu CCM wana misimamo yao kuhusu Rasimu ya Katiba na wamekuwa wakikutana na kutoa maoni tofauti na Rasimu ya Katiba. Tulipobaini hilo, tukaona ni busara kuanzisha Ukawa ili kutetea maoni ya wananchi katika rasimu.
Swali: Je, umoja huu una jumla ya wanachama wangapi?
Jibu: Umoja huu ulianzishwa ukiwa na wanachama 203 na hadi sasa tuna jumla ya wanachama 286, kati yao kuna wabunge wanne wa CCM na tunatarajia wanachama kuongezeka zaidi.
Swali: Je, umoja huu unaongozwa na kina nani, baada ya kupata wazo na kuanzishwa?
Jibu: Ukawa ulichagua viongozi wa muda. Mwenyekiti ni James Mbatia na mimi ni katibu. Pia kuna wenyeviti wenza kama Profesa Ibrahim Lipumba na Freeman Mbowe na yupo Tundu Lissu na wengine wengi.
Swali: Je, mna mpango wa kufanya uchaguzi ili kuwa na viongozi wa kudumu hadi mwisho wa Bunge hili maalumu?
Jibu: Ndiyo hivi sasa tunajiandaa kwa uchaguzi ambao tunahitaji ukusanye makundi yote yenye uwakilishi hapa bungeni ili kuwa na sauti ya pamoja.
Swali: Katika siku za karibuni Ukawa mmekuwa mkitajwa kuwa sehemu ya makundi ambayo yanaweza kuleta vurugu bungeni nini maoni yako?
Jibu: Hapana, sisi malengo yetu makubwa ni kutetea hoja za wananchi, kanuni za bunge na taratibu bila kujali misimamo ya vyama vyetu. Sasa unavyofanya hivyo kila mtu anatafsiri yake, lakini wanaojua ukweli wameona mchango wetu katika katiba hii.
Swali: Ni jambo gani kubwa ambalo mnadhani Ukawa mmefanya tangu kuanza kwa Bunge maalumu la katiba?
Jibu: Tumefanya mengi lakini, kubwa lilikuwa ni kushinikiza Jaji Warioba kupewa muda wa kutosha katika kuwasilisha Rasimu ya Katiba, kama ambavyo uliona Mwenyekiti alivunja Kanuni ya 47(a) ambayo ilimtaka afanye mawasiliano na Jaji Warioba ili kumpangia muda ambao unafaa kusoma rasimu.
Lakini Mwenyekiti alimpangia saa moja tu na baada ya malalamiko yetu, aliongeza saa mbili. Tulipinga na hata kusababisha kusitishwa Bunge siku ambayo Jaji Warioba alipangiwa kuwasilisha rasimu ya pili.
Swali: Kwa nini mlizuia Jaji Warioba kusoma rasimu na baadaye mkaja kukukubali?
Jibu: Naomba hapa nieleze Ukawa ilikuwa haimzuii Jaji Warioba kusoma Rasimu, ila ilitaka apewe muda wa kutosha kwani tulijua muda wa saa mbili yasingetosha na ukweli baadaye ulijionesha alitumia zaidi ya saa tatu.
Lakini kabla ya uamuzi huo, tuliomba kuonana na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Samuel Sitta ambaye alitupuuza na hata tulipoandika barua pia alipuuza na tulikuwa hatuna njia nyingine ya kumpatia fursa nzuri Jaji Warioba zaidi ya sote kusimama bungeni.
Pia tulikuwa na hoja ya kupinga kuvunjwa kanuni ya 71(1)(g) na (h) ambayo ilitaka Baada ya Rais Jakaya Kikwete kuzindua bunge ndipo Jaji Warioba awasilishe rasimu.
Swali: Je maombi yenu baada ya kusitishwa bunge yalifanikiwa.
Jibu: Tulifikia maridhiano ambayo yamekuwa na manufaa makubwa kwa Watanzania,kwani Jaji Warioba alipewa muda wa kutosha kuwasilisha rasimu na Katiba ya Rais kuendelea kama awali hapa ilikuwa ni “Give and take” na hapo ndio utaona umuhimu wa kuwa na chombo kama Ukawa.
Swali: Baada ya Jaji Warioba kuwasilisha rasimu je imekidhi matakwa yenu?
Jibu: Jaji Warioba na tume yake wamefanya kazi kubwa sana na hakika wamewasilisha bungeni maoni ya wananchi na sisi tumeridhika.
Swali: Katika siku za Karibuni zimepitishwa kanuni za bunge kuhusiana na masuala ya nidhamu bungeni na Mwenyekiti wa bunge, ameonya kuchukuliwa hatua kali kwa watakaoleta vurugu ni nini maoni yako?
Jibu: Ni kweli tumepitisha kanuni na hatuna shida na hili, lakini tuna matatizo na kauli za vitisho ambazo zinatolewa. Kwanza hapa lazima ieleweke sote sisi ni watu wazima hivyo, mambo ya kutishana si vizuri.
Swali: Kwa hiyo mtaendelea kusimamisha bunge kwa kusimama na kuomba miongozo kama kanuni zikikiukwa?
Jibu: Kama nilivyosema awali tutahakikisha tunasimamia kanuni na taratibu hivyo hatutakubali kuburuzwa kwani sisi tunawakilisha wananchi na kutetea maoni yao yaliyopo kwenye rasimu pia kanuni na taratibu ambazo tumejipangia.
Huu ndio Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) lakini je utafikia malengo yake ya kutetea kile wanachokieleza maoni ya wananchi yaliyopo kwenye rasimu ya Jaji Warioba, tusubiri vikao vya bunge vinavyoendelea.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa