Home » » Jaji Mchome aipongeza Tume ya Warioba

Jaji Mchome aipongeza Tume ya Warioba

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Lawrence Mchome ameipongeza Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa kukubali kuingiza katika Katiba Mpya ibara inayotaka kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu nchini.
Kama itapitishwa, mahakama hiyo itakuwa ndiyo ngazi ya mwisho ya rufaa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pamoja na mambo mengine, mahakama hiyo itasikiliza na kuamua mashauri yanayohusu matokeo ya uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Pia itasikiliza na kuamua mashauri yatakayowasilishwa na wananchi, Serikali au Serikali za washirika kuhusu tafsiri au utekelezaji wa Katiba Mpya kama itapitishwa na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.
“Kenya na Uganda wanayo mahakama kama hiyo kwa hiyo sisi (Tanzania) tulikuwa tukienda Mahakama ya Rufaa ya Afrika Mashariki, tulionekana wanyonge kwa sababu tumeishia hatua mbili za rufaa,” alisema Jaji Mchome.
Jaji Mchome, ambaye ni rais wa zamani wa Chama cha Mahakimu na Majaji Afrika Mashariki (EAMJA), alisema kuwapo kwa mahakama hiyo kutasaidia kuweka utawala sawa wa sheria katika nchi za Afrika Mashariki.
“Wenzetu Kenya na Uganda wana hatua tatu za rufaa kabla ya kufika Mahakama ya Rufaa ya Afrika Mashariki, lakini sisi tuna mbili tu; Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama ya Rufaa,” alisema Jaji Mchome.
Jaji Mchome alisema kama ibara hiyo itapitishwa na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, itaifanya Tanzania kuwa na hatua za sheria zinazolingana na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
“Hata mitalaa ya vyuo vya sheria katika nchi zetu za Afrika Mashariki, zinatakiwa zifanane sambamba na nchi hizo kuwa na hatua za rufaa zinazofanana kati ya Kenya, Tanzania, Uganda, Rwanda na Burundi,” alisema.
“Tukishafanya hivyo, tutakuwa tumepatanisha haki na uendeshaji wake na kufanya hatua zote za sheria zilingane na hivyo haki itakayokuwa inatolewa kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki italingana,” alisisitiza.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa