Home » » 'CDA INAWATESA WANANCHI, IVUNJWE'

'CDA INAWATESA WANANCHI, IVUNJWE'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi juzi alipata wakati mgumu kwenye mkutano baada ya wananchi na baadhi ya madiwani kukataa hoja zake mbele ya Rais Jakaya Kikwete.
Hatua hiyo ya wananchi, ilikuja baada wa Mbunge wa Dodoma Mjini, David Malole (CCM) kusema Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) imekuwa ikifanya maonevu mengi kwa wananchi, ikiwemo kubomoa nyumba, makanisa kutaka ardhi irudi Manispaa.
Pia, Mbunge huyo alisema hivi karibuni CDA ilibomoa makaburi ya Wazee wa Kimila eneo la Iyumbu na kusababisha mifupa ya marehemu hao kuzagaa ovyo, jambo ambalo halileti picha nzuri.
Alisema eneo hilo ambalo ni la kihistoria, lilitakiwa kutunzwa, lakini badala yake limebomolewa licha ya Chifu wa kabila la Kigogo, Lazaro Chihoma kufanya juhudi mbalimbali za kutaka eneo hilo, litangazwe kuwa na kihistoria.
Alisema eneo hilo, limekuwa likitumika na hukutanisha watu zaidi ya 2,000 kila mwaka kwa ajili ya matambiko. Pia, alisema CDA imekuwa ikibomoa nyumba za wananchi bila taarifa na wakati mwingine kubomoa nyumba usiku, hali inayokera wananchi wengi.
“CDA iondolewe, halmashauri nyingi zimekuwa Majiji bila CDA, CDA inawatesa wananchi, hawa unaowaona hapa ni wabomolewaji watarajiwa” alisema Mbunge huyo huku akishangiliwa na wananchi.
Baada ya kauli hiyo, Waziri Lukuvi ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya CDA alipanda jukwaani kwa ajili ya kusalimia wananchi na kubainisha kuwa CDA ni taasisi kama ilivyo Manispaa. Alisema ndani ya CDA kuna utendaji usioridhisha.
“Yaliyosemwa na Mbunge tumeyasikia, yuko mkuu wa Mkoa, Mwenyekiti wa CCM, Meya, niko tayari kuitisha bodi na kubariki maneno yote yaliyosemwa na Mbunge uamuzi utakaotolewa na kikao cha Mkuu wa Mkoa akiwemo Mbunge na Meya wa Manispaa,” alisema Waziri Lukuvi huku wananchi wakimtaka kushuka jukwaani.
Hata hivyo, Lukuvi alisema hana uwezo wa kuivunja CDA, ila ana uwezo wa kuondoa kero za CDA.
Wananchi hao waliendelea kupiga kelele na kumtaka Waziri Lukuvi kushuka jukwaani, ambapo alishuka na kuelekea jukwaa kuu.
Baada ya kupanda jukwaani, Rais Kikwete alisema kama ingekuwa siku ya kupiga kura, Mbunge huyo mambo yake yangekuwa mazuri.
“Leo pamenoga kweli hapa, kama ingekuwa siku ya kupiga kura leo, Malole mambo yako yangekuwa mazuri, unaposema unashangiliwa sana,” alisema Rais Kikwete.
Alisema kinachotakiwa kufanyika ni bodi ya CDA kukutana na bodi ya Mkoa Manispaa, Mbunge, kamati ya mipango Miji kukaa katika mkutano wa pamoja.
Alisema huo utakuwa ni mkutano wa kazi na unatakiwa kuwa na watu wachache; na hata madiwani wasiwepo hapo.
“Kupiga zogo hakusaidii, majawabu huwa hayapatikani kwenye mkutano wa Hadhara, lazima watu wakae wajue tatizo ni nini na nipatiwe majibu Septemba 7,” alisema Rais Kikwete.
Chanzo;Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa