Home » » SITTA: MAASKOFU NI UKAWA

SITTA: MAASKOFU NI UKAWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba,Samuel Sitta


Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Samuel Sitta sasa ‘ametangaza rasmi vita’ dhidi ya viongozi wa dini kwa kusisitiza kuwa hayuko tayari kuwaheshimu wala kuwavumilia  ambao wanatoa nyaraka alizodai kuwa hazina utukufu wa Mwenyezi Mungu kwa waumini wao.

Sitta alitoa kauli hiyo jana asubuhi bungeni wakati akisoma matangazo mbalimbali na kuamua kusoma waraka aliodai kuwa umetolewa na viongozi hao wa dini huku akiuhusisha na siasa za kundi la wajumbe waliosusia Bunge Maalum la Katiba kutoka Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi.

Kundi hilo limejitambulisha kama Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Alisema katika mitandao ya kijamii amekuwa akituhumiwa kuwa anawadharau maaskofu, huku akidai kuwa wakiendelea na matendo kama hayo kamwe hatawaheshimu.
“Wakiwa na matendo kama hayo, hao maaskofu, itabidi wengine tuendelee kuwadharau tu, ninao waraka huu ambao umelazimishwa kusomwa ndani ya makanisa, sioni utukufu wala Ukristo ndani ya waraka huu,” alisema Sitta.

Alisema kuwa maneno na ujumbe uliomo ndani ya waraka huo unashabihiana na malengo ya kundi la wajumbe waliounda Ukawa na kususia vikao vya BMK.
Akisoma baadhi ya vipengele vya waraka huo, Sitta alisema kuwa sehemu ya waraka huo unamlazimisha Rais airudishe Tume ya Mabadiliko ya Katiba na asitishe mchakato wa Katiba, huku akihoji:

“Tangu lini watu wa kiroho wanatoa maagizo ya mambo ya siasa, hii siyo haki hata kidogo, lugha iliyoandikwa humu ni lugha ya wale tulio wazoea ukawa.” 

Hata hivyo, baadhi ya wajumbe walilazimika kuomba mwongozo wa Mwenyekiti, na walipopewa walimshauri Sitta kupatana na viongozi wa dini kisha awaombe wamuombee kwa Mungu kwa kazi anayoifanya. Mbunge wa Kishapu, Seleman Nchambi, alisema kuwa anatilia shaka waraka uliosomwa na Sitta kama kweli ameutoa kwa viongozi wa dini na badala yake akasema huwa huwenda waraka huo umeokotwa baada ya kuandaliwa na wahuni.

“Sina imani na siamini kama kiongozi wa dini aliyesoma torati, akasoma Injili, akasoma Quroan na akasoma Biblia, anaweza akayasema maneno hayo katika nyumba ya Mungu, lakini kama ikitokea na kama imetokea yamesomwa, basi tusifanane na hao kwa kuwa Mungu anajua tunachokihitaji kabla haya kumwomba,” alisema Nchambi.

Akitoa mwongozo kwa Nchambi, Sitta alipuuza ushauri aliopewa na badala yake aliishia kumsifia Mbunge huyo kwa kujitahidi kusoma na kuielewa Biblia na Quroan.

Kwa upande wake Mjumbe wa BMK kupitia kundi la 201, Oliva Lwena alimuasa Sitta kutowachukia viongozi wa dini kutokana na yale yanayotokea ndani ya Bunge akisema kuwa huwenda viongozi hao wanapotoshwa na baadhi ya vyombo vya habari au baadhi ya wajumbe waliosusia vikao vya bunge hilo.

Badala yake alimtaka baada ya kumalizika kwa shughuli za BMK afanye ziara ya kutembelea madhehebu mbalimbali ya dini kama alivyofanya wakati akianza kuongoza Bunge hilo ili kuwaeleza viongozi wa dini hizo mambo yaliyokuwa yakifanywa na BMK.

“Wakati ukianza kuliongoza Bunge hili ulifanya ziara ya kuwatembelea viongozi wa dini, hilo lilikuwa jambo jema, inawezekana viongozi hao hawajui tunachokifanya humu ndani na badala yake wanapata taarifa kupitia vyombo vya habari au wanapotoshwa na wajumbe waliosusia bunge hili, nakushauri baada ya shughuli za Bunge hili urudi tena kufanya ziara ya kuwatembelea ili uwaeleze tulichokuwa tunakifanya humu ndani,” alisema Lwena.

CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa