Home » » Bilioni 43.89 zatumika kusambaza umeme Dodoma

Bilioni 43.89 zatumika kusambaza umeme Dodoma



Na Greyson Mwase, Dodoma

Meneja wa Shirika la Umeme Nchini  (Tanesco) mkoa wa Dodoma, Zakayo Temu amesema kuwa Serikali imetenga  jumla ya shilingi  bilioni 43.89 kwa ajili ya kujenga miundombinu ya  umeme katika mkoa wa Dodoma kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Awamu ya Pili.

Temu aliyasema hayo mbele ya Kamati ya Kudumu  ya Bunge ya Nishati na Madini  iliyopo  mkoani  Dodoma kwa ajili ya kukagua miradi  ya umeme  ili kujionea utekelezwaji wake pamoja na kuzungumza na wawakilishi wa wananchi. Mbali na mkoa wa Dodoma, kamati hiyo  inatarajia kufanya ziara ya kukagua miradi ya umeme katika mikoa  ya Singida, Arusha na Kilimanjaro pamoja na   kuzungumza na wadau wa madini katika mkoa wa Manyara.

Akitoa  taarifa ya utekelezaji wa miradi ya umeme katika mkoa wa Dodoma chini ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Awamu ya  Pili, Temu alisema kuwa mradi  kabambe wa kusambaza umeme  vijijini  awamu ya pili  unahusisha wilaya  zote za mkoa wa Dodoma, wilaya za Chamwino, Kongwa zikiwa mojawapo.

Akielezea kazi ya usambazaji wa umeme katika wilaya  ya Chamwino  Temu alisema kazi ya kupeleka umeme  itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti 33 urefu wa kilomita 171.5 na  njia ya msongo  wa kilovoti 0.4 urefu wa kilomita 95.

Alisema  ujenzi utahusisha pia ufungaji wa transfoma 22 za ukubwa mbalimbali  pamoja na kuunganisha wateja wapatao 1,195 kwa gharama inayokadiriwa kuwa shilingi za kitanzania bilioni 8.67.

Aliongeza kuwa katika wilaya ya  Chamwino  hadi sasa ujenzi wa miundombinu  ya umeme  umefikia asilimia 52 na wateja 105 kati ya 1,195 wamekwisha unganishwa na huduma ya  umeme na kusisitiza kuwa mradi huu  unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu.


Alitaja maeneo yatakayofaidika na umeme huu kuwa ni pamoja na  vijiji  vya  Fufu, Masanze, Mloda, Handari, Chololo, Kikombo, Igandu, Msanga, Chinangali, Mwegamile, Mpera,  Chamwino Ikulu,  Solowu, Zajilwa,  Segala, Izava, Itiso, Magungu, Osteti, Dabalo, Nzali, Majeleko, Mlimwa, Igamba, Membe na Ikowa.

Alitaja  vijiji  vingine ni pamoja na Msamalo, Makoja, Mnase, Mgunga, Mlebe, Ndebwe, Handali, Chanhumba, Matumbulu, Igogi, Chaludema, Sazima, Nkowe,  Chinyika, Chinyanguku, Nghaheleze, Ikombolinga, Idifu, Miganga, Muungano, Ilolo, Chalinze B, Azimio B na  Shule ya Msingi  Chinangali II

Wakati huo huo akielezea hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa miundombinu ya umeme katika  wilaya ya Kongwa, Temu alieleza  kuwa kazi ya kupeleka umeme katika wilaya hiyo inahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti  33 urefu wa kilomita 197 na  njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 urefu wa kilomita 66.

Alisema  pia ujenzi huo unahusisha  ufungaji wa transfoma 51 za ukubwa mbalimbali  pamoja na kuunganisha wateja wapatao 1,195 kwa  gharama inayokadiriwa kuwa shilingi za kitanzania bilioni 9.24

Alisema hadi kufika sasa ujenzi wa miundombinu  ya umeme umefikia kwa asilimia 68 na wateja 30 kati ya  1,640 wamekwisha unganishiwa umeme na kusisitiza kuwa mradi huo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu.

Alitaja vijiji  vitakavyonufaika na mradi huo kuwa ni pamoja na Manguto, Matongoro, Nororia, Mlanje, Manyata, Ngomai, Njoge,  Chiwe, Moleti, Pingakame,  Mlanje, Sejeli, Mkutani, Banyibanyi, Mageseni, Makawa, Mkoka na Magereza Vijiji vingine ni pamoja na Nilini, Ndurugumi,  Laikala, Mlali Ng’umbi, Mranana, Chingwilingwili, Ndalibo, Zoissa na Chitego.

Akielezea changamoto katika utekelezwaji wa mradi wa REA  Awamu ya  Pili  Temu alieleza kuwa ni pamoja na wananchi wengi kuhitaji  huduma ya umeme katika awamu hiyo japokuwa  hawapo kwenye mpango huo  kwa sasa na  njia ya umeme  kutembea kwa umbali mrefu sana kupita kiwango cha kawaida na hivyo kuwa na  viashiria vya kupata umeme mdogo kwa muda mfupi. Aidha, alisisitiza kuwa katika utekelezaji wa mradi, baadhi ya wananchi wamekuwa wakijitokeza kudai  fidia.

Alisema  ili kutatua changamoto hizo  kama shirika la Tanesco litaendelea kubaini maeneo  ambayo  yanahitaji umeme ili yawekwe kwenye  bajeti ya Tanesco inayoandaliwa kila mwaka na kwenye maeneo  ya  vijijini  shirika litaendelea kuweka miradi ya  REA kwa kadri itakavyokuwa inahitajika lengo likiwa ni kuhakikisha kila mwananchi anafurahia  huduma ya umeme.
“Pia tutaendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa miradi ya umeme   hususan  vijijini kwa maendeo ya taifa ili kuondokana na dhana ya kudai  fidia ambayo ni kubwa  kuliko  bajeti iliyotengwa”, alisisitiza Temu.

Chanzo Jiachie Blog


Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa