Home » » CCM MPWAWA YAKANUSHA.

CCM MPWAWA YAKANUSHA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na Urban Epimark,Mpwawa.
HALMASHAURI ya Wilaya ya Mpwawa imekanusha vikali taarifa kwamba BARAZA LA Madiwani wa Halmashauri hiyo limetunga sheria mpya ya tuzo mbalimbali kinyemela ili kuwazibiti wafanyabiashara wanaoegemea upande wa upinzania.
Hayo yalielezwa juzi na Kaimu Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mpwawa, ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Chunyu, Mhe Neemia Kongawadodo kwenye mikutanao ya hadhara iliyofanyika katika kata za Mlunduzi, Luhundwa na Wota Jimbo la Kibakwe wilaya ya Mpwawa.
Diwani huyo aliyemwakilisha Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mhe Alex Buramulete Nyaulingo aliwaambia wananchi kwamba, hakuna sheria yeyote iliyotungwa na kupitishwa na Baraza la Madiwani hivi karibuni inayokusudia kutoza malipo kwa wananchi mbalimbali wanaojihusisha na biashara za bodaboda, mafundi pikipiki na baiskeli, mama na babalishe au tozo za uvunaji miti au mbao.Alisema hizo ni mbinu za baadhi ya watu wasioitakia mema halmashauri hiyo katika utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ambapo baraza hilo la Madiwani lote lipo chini ya mwavuli wa Chama cha Mapinduzi.
Aliendelea kusema, baraza hilo limekuwa siku zote likitunga na kupitisha sheria ndogondogo katika halmashauri hiyo na kuziweka wazi hadharani kwa kufuata taratibu za kisheria zilizowekwa, sasa iweje muda unafikia mwisho wa utekelezaji wa Ilani yake, yaanze kuibuka malalamiko kama hayo. Alieleza Diwani Kongawadodo.
Nae Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Mpwawa Bw Origenesi John alikitetea chama kwa kueleza kwamba, “wale wote wenye tamaa ya kuwania baadhi ya nafasi za uongozi kwa ngazi ya Udiwani na Ubunge katika uchaguzi mkuu ujao kupitia Chama Cha Mapinduzi kuacha kufanya hivyo sasa kwani muda wa kamapeni bado haujaanza.
Alisema, “waacheni madiwani wetu pamoja na wabunge watekeleze kwa ukamilifu jukumu walilokabidhiwa na chama, bila kuwaingilia”. Aliendelea kusema huku akinukuu vifungu vya kanuni za uchaguzi kwenye katiba ya CCM kwamba, wanaofanya hivyo wanajipunguzia sifa za kuwa wagombea, na wakati ukifika watapoteza sifa za kuteuliwa.
Aliendelea kuainisha kwamba, CCM imegundua inao wanachama wengi wanaokusudia kuwania nafasi mbalimbali kwenye uchaguzi ujao, lakini amewashauri wavute subira hadi muda utakapofika. “Kuendelea kupotosha wananchi kwa kutoa kauli au shutuma kwa viongozi waliopo madarakani hivi sasa hakutasaidia, kwani hali halisi inajidhiirisha kwamba chama kwa kushirikiana na wabunge wao na madiwani wamefanya mambo mengi na makubwa, hivyo wasijidanganye”, alieleza katibu mwenezi huyo.
Aliendelea kuainisha jinsi walivyoshirikiana na halmashauri ya Mpwawa pamoja na Mbunge wao wa  Kibakwe, Mhe George Simbachawene, ambaye pia ni Waziri wa Nishati na Madini kuwaletea wananchi maendeleo katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo ikiwemo ukarabati wa barabara, usambazaji wa umeme kupitia REA, ujenzi wa shule na maabara, ujenzi wa zahanati na kuhakikisha upatikanaji wa vifaa tiba husika na mengine mengi.
Aliendelea kueleza katika mikutano hiyo, ambapo yeye alijigamba kuendelea “kuporomosha mawe ya ukweli kwa wapinzania” kwamba ukarabati wa gari la shule ya sekondari ya Wota iliyopo Kata ya Wota, Jimbo la Kibakwe, uliofanikishwa kwa kiwango cha juu kabisha na mbunge wa Jimbo hilo, ambapo gari hilo aina ya Toyota Land Cruiser lenye usajili Na. STJ 5656 la Shule ya Sekongari ya Wota, lilikaa  gereji kwa miaka 5 kutokana na ukosefu wa fedha za kulikomboa lakini Mbunge huyo kwa kusaidiana na wananchi wa Kibakwe wamefanikiwa kulipa na kukuomboa gari hilo baada ya kulipia gharama ya shilingi milioni 17, na sasa amelikabidhi kwa Mkuu wa shule hiyo.
Aliendelea kuwapinga wapinzani kwamba, usambazaji wa umeme katika kata hizo  pamoja na ujenzi wa zahanati ya Wota, ujenzi wa barabara za kutoka Kibakwe mjini hadi maeneo mbalimbali ya Kata za Mlunduzi,Luhundwa na Wota pamoja na upatikanaji wa dawa kwenye zahanati husika, ni salamu tosha kwamba CCM imetekeleza vyema ahadi zake za kuwaletea wananchi maisha bora kwa kila mtanzania, hivyo wasiwabeze viongozi waliopo madarakani hivi sasa, alieleza.
Chama cha Mapinduzi wilaya ya Mpwawa, kilijumuika katika ziara ya  mbunge wa Jimbo la Kibakwe, kukagua maendelea ya miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa chini ya Ilani ya chama, ikiwamo mradi wa usambazaji umeme vijijini kupitia REA. Mafanikio makubwa yamefikiwa na TANESCO hadi sasa katika harakati za kusambaza umeme vijijini.
    

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa