WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk Harrison Mwakyembe amesema Rais
Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete hakutumia ibara ya 45 ya Katiba
kutoa msamaha kwa baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi katika Akaunti ya
Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu (BoT), wanaoelezwa
kuamriwa kurejesha fedha walizochukua.
Aidha, alisema pale ambapo kuna makosa, Rais anaweza kumsamehe mtu
ambaye tayari amehukumiwa au kupewa adhabu kwa kutumia ibara hiyo.
Alisema, “Mimi kwa taarifa nilizonazo Mheshimiwa Rais mstaafu
hakutumia kifungu hicho,” Dk Mwakyembe alisema bila kueleza kifungu
kilichotumiwa.
Alisema hivyo jana bungeni mjini hapa, wakati akijibu swali la
nyongeza la Mbunge wa Konde, Khatib Said Haji (CUF) aliyetaka kujua
endapo Rais aliyepita alitumia madaraka yake vibaya, alikosea au alikuwa
sahihi kuruhusu baadhi ya watuhumiwa walipe fedha walizodaiwa
kuzifanyia ubadhirifu kupitia akaunti ya EPA (Hawakutajwa).
Pia, mbunge huyo katika swali lake la pili la nyongeza alitaka kujua
ni lini watafikishwa mahakamani akieleza kuwa msamaha waliopewa haukuwa
wa kikatiba na kwamba wanastahili kushitakiwa.
Katika swali lake la msingi, Haji alitaka kujua iwapo Rais ana
mamlaka ya kisheria kutoa msamaha kwa watuhumiwa wa uhalifu wa aina
yoyote ambayo mashauri yake yapo katika vyombo vya dola kwenye hatua za
uchunguzi, upelelezi au mahakamani.
Alisema kwa mujibu wa Ibara ya 45 (1, A hadi D) ya Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Rais ana mamlaka ya kutoa msamaha kwa wafungwa
waliopo gerezani.
Akijibu, Dk Mwakyembe alisema, ibara hiyo inampa Rais mamlaka ya
kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia mbele ya mahakama.
Mamlaka mengine ni kumwachilia kabisa au kwa muda maalumu mtu yeyote
aliyehukumiwa kuadhibiwa kwa ajili ya kosa lolote. Pia ana mamlaka
kubadilisha adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa kosa lolote iwe
adhabu tahafifu pia anaruhusiwa kufuta adhabu yoyote au sehemu ya
adhabu.
Alisema, kwa kuzingatia masharti hayo ya Katiba, msamaha wa Rais
unatolewa kwa mtu aliyetiwa hatiani na kupewa adhabu na mahakama.
“Watuhumiwa wa uhalifu ambao mashauri yao yako katika hatua ya
upelelezi au uendeshaji mahakamani hawaguswi na masharti ya ibara hii.
Kwa sababu hiyo, Rais hawezi kisheria kutoa msamaha kwa watuhumiwa wa
uhalifu wa uhalifu wa aina yoyote ambao mashauri yao yapo katika vyombo
vya dola kwenye hatua za uchunguzi, upelelezi au mahakamani,” alisema Dk
Mwakyembe.
Aliongeza kuwa, hatma ya watuhumiwa hao inakuwa bado ipo katika mamlaka husika za uchunguzi, mashitaka na mahakama.
Chanzo Gazeti La Habari Leo
0 comments:
Post a Comment