Home » » AWESO AWATAKA WAKANDARASI KUWA WAZALENDO

AWESO AWATAKA WAKANDARASI KUWA WAZALENDO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Jumaa Aweso akizungumza na wananchi wa kijiji cha Bubutelo wilayani Chemba.


Mbunge wa Chemba Juma Nkamia akizungumza na wananchi wa Bubutelo katika ziara ya Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Jumaa Aweso.

Wananchi wa Bubutelo wilayani Chemba wakimsikiliza Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Jumaa Aweso.

Naibu waziri wa maji na umwagiliaji Jumaa Aweso amewataka wakandarasi nchini kuwa wazalendo katika kuhakikisha fedha zinazopelekwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji zinafanya kazi iliyokusudiwa.

Aweso ametoa rai hiyo akiwa katika kijiji cha Bubutelo wilayani Chemba akiwa katika ziara yake ya kutembelea na kuzumgumza na wananchi wa vijiji vya Mombose na Bubutelo ambavyo vipo katika eneo linalotarajiwa kujengwa bwawa la Farkwa.

Aweso amesema serikali inajitahidi kutenga fedha ili kukamilisha miradi hiyo na hatimaye ifikie azma ya kumtua ndoo ya maji kichwani kama ilivyokusudiwa hivyo ni wajibu wao kuwa wazalendo.

"Mkandarasi anayepewa kazi ajione kabisa yeye ni Mtanzania avae uzalendo kwa Taifa lake,serikali inatenga fedha nyingi za miradi lakini wapo wakandarasi ambao sio waaminifu jambo ambalo linakwamisha nia nzuri ya serikali iliyonayo,"amesema Aweso.Katika ziara hiyo Aweso amesikiliza vilio vya wananchi ambao wengi waliomba kujua hatma ya fidia zao ili wapishe mradi huo suala ambalo amesema linashughulikiwa na likikamilika kila anayestahili kulipwa atalipwa.

Kwa upande wake mbunge wa Chemba Juma Nkamia amesema wananchi wameupokea mradi huo vizuri na wanachosubiri ni fidia zao na kuwasisitiza wananchi kuwapuuza baadhi ya watu wanaopita na kusema mradi huo haufai.Naye kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Jofrey Pima amesema hali ya upatikanaji wa maji ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya watu waliokuwepo ambapo mijini wananchi 4490 ndio wanapata maji na kijijini ni asilimia 44.

"Bwawa la Farkwa likikamilika litasaidia kuongeza idadi ya wanaopata maji na hivyo kukidhi dhamira ya serikali,kwa sasa upembuzi yakinifu umeshafanyika,tunasubiri suala la kuwalipa fidia wananchi,"amesema kaimu mkurugenzi huyo.Wilaya ya Chemba ilianzishwa mwaka 2012 na mwaka 2013 iliundwa halmashauri ambapo ina jumla ya tarafa 4,kata 26 na vijiji 114 ikiwa na jumla ya wakazi laki 256,623 kwa sasa.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa