Home » » WAZIRI SIMBACHAWENE AIPONGEZA TARURA KUFUNGUA BARABARA KWENYE MILIMA MIKALI KATA YA MANG’ALIZA

WAZIRI SIMBACHAWENE AIPONGEZA TARURA KUFUNGUA BARABARA KWENYE MILIMA MIKALI KATA YA MANG’ALIZA


#Barabara za zege zaonesha ufanisi, zafungua maendeleo   

#TAMISEMI kuhakikisha mlima huo unaboreshwa na kupitika muda wote

Na. Catherine Sungura, Kibakwe - Mpwapwa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mbunge wa Kibakwe, Mhe. George Simbachawene  ameishukuru na kuipongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA)  kwa kuanza kujenga barabara za zege kwenye milima mikali iliyopo kata ya Mang’aliza-Kibakwe wilayani Mpwapwa.

Waziri Simbachawene ameyasema hayo wakati wa ziara  ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu inayosimamiwa na TARURA  iliyofanywa na Naibu Katibu Mkuu wa OR-TAMISEMI anayeshughulikia miundombinu  Mhandisi Rogatus Mativila .

“Niwashukuru sana TARURA na kuwapongeza kwa kutusaidia tulio kwenye mazingira magumu, jimbo langu la Kibakwe lipo katika maeneo tambarare na milimani, na hii ni milima mikali ambayo ipo karibu kata sita na hakuna namna yoyote ya kutengeneza barabara zaidi ya barabara za zege”.

Ameongeza kusema kuwa utaratibu huo wa TARURA wa kujenga barabara za zege  waliouanza miaka michache iliyopita umeanza kuleta ufanisi mkubwa hususani kufungua maendeleo pamoja na kuwaletea huduma nyingine wananchi ikiwemo umeme, shule ya sekondari pamoja na kituo cha afya.

“Kata ya Mang’aliza haikuwa na maendeleo kabisa lakini hii  barabara ilivyofunguliwa hivi karibuni imeleta maendeleo kwa wananchi kwani miaka ya nyuma nilikuwa nakuja huku kwa pikipiki  lakini sasa hivi nakuja kwa gari na hata magari makubwa yanafika kuleta vifaa vya ujenzi ambapo kuna shule ya sekondari inajengwa, kwasababu sehemu korofi zote wameweka zege, kwakweli nawapongeza TARURA”, aliongeza Mhe. Simbachawene.

“Hata hivyo ombi langu tu waendelee kutenga fedha kwa maeneo mengine kwani Ilani na sera  yetu sasa ni kuwapelekea umeme na huduma nyingine wananchi lakini  changamoto ilikuwa ni barabara ila kusema ukweli TARURA wamejitahidi sana kwani fedha zinazohitajika ni nyingi ila kwa hicho kidogo wamefungua hizo barabara na sasa zinapitika na shughuli za kijamii zinaendelea kama kawaida" alisisitiza. 

Aidha, Mhe. Simbachawene  aliwapongeza  Mhe. Rais  Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhangaika kutafuta  rasilimali fedha, watendaji wa TARURA kwa kazi nzuri pamoja na TAMISEMI kwa usimamizi ambapo ana imani nia ya kufungua barabara zaidi itaendelea.

Naye, Naibu Katibu Mkuu OR-TAMISEMI Mhandisi Rogatus Mativila amesema mlima huo wenye urefu wa Km. 5 umekuwa mgumu sana kupitika wakati wa kiangazi na hata masika ambapo chini ya mlima huo  kuna uzalishaji mkubwa kutoka kwa wafugaji na wakulima wa mazoa mbalimbali ambapo TARURA  wameweza kutengeneza maeneo korofi kwa kujenga barabara za zege la saruji lililochanganywa na kototo pamoja na nondo ambapo hivi sasa barabara hiyo inapitika.

Mhandisi Mativila amesema kwamba wao kama OR-TAMISEMI wataendelea kuhakikisha mlima huo unaboreshwa na kupitika muda wote na kuahidi kuendelea kutoa fedha zaidi ili wananchi waendelee kuzalisha mazao mbalimbali  na kupatiwa huduma za kijamii ikiwemo shule na afya.

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa